WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, February 24, 2013

Simba yaweka rehani ubingwa




JAHAZI la Simba limeendelea kuzama baada ya kukubali kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Mtibwa Sugar katika mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara iliyofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Beki Salvatory Ntebe aliifungia Mtibwa Sugar bao pekee katika dakika ya 18 akiunganisha vizuri pasi nzuri ya Vicent Barnabas katika mchezo huo ambao Simba walimaliza wakiwa 10 baada ya beki Juma Nyoso kupewa kadi nyekundu katika dakika ya 86.

Kwa matokeo hayo Simba imebaki ikiwa nafasi ya tatu na pointi zake 31, huku Yanga wakiendelea kuongoza wakiwa na pointi 39, wakifuatiwa na Azam (36) katika mbio hizo za kusaka ubingwa.
Kocha wa Simba, Patrick Liewig alisema nafasi ya timu yake kutwaa ubingwa ni ndogo kwa sasa kutokana na matokeo hayo.
“Uchovu wa safari ndefu iliyoifanya timu yake hivi karibuni mikoani na kucheza mechi za mfululizo ni sababu ya kupoteza mchezo wa leo,” alijitetea kocha huyo.

Naye Mecky Mexime aliwasifu wachezaji wake kwa kucheza vizuri na kufanikiwa kupata ushindi huo mzuri dhidi ya Simba.
Katika mechi hiyo dakika ya pili, beki Amir Maftah alipitisha krosi nzuri kwa Shomari Kapombe aliyepiga shuti kali lililopaa juu ya lango la Mtibwa Sugar.

Katika dakika ya 18, pasi ya Barnabas ilimkuta Ntebe aliyepiga shuti kali lililomshinda kipa Juma Kaseja na kujaa wavuni hivyo kuipa Mtibwa Sugar bao la kuongoza.

Kuingia kwa bao hilo kuliamsha ari ya Mtibwa Sugar kwani katika dakika ya 23, shuti la mshambuliaji Hussein Javu lilipanguliwa kwa ustadi mkubwa na kipa Kaseja.

Simba ilijaribu kurudi mchezoni katika dakika ya 28, ambapo Felix Sunzu alipiga shuti kali, lakini lilipaa juu ya lango la Mtibwa.
Katika mchezo huo kocha wa Simba, Liewig hakuwaanzisha wachezaji wake mahiri, Amri Kiemba pamoja na Mrisho Ngassa, lakini baadaye alifanya mabadiliko kwani aliwatoa Ramadhani Chombo, Haruna Moshi na Haruna Chanongo na kuwaingiza Kigi Makasi, Kiemba na Ngassa.

Katika hali ya kushangaza wachezaji Chombo na Moshi baada ya kutolewa walikwenda moja kwa moja kwenye vyumba vya kubadilishia nguo badala ya kukaa katika benchi.

Pamoja na mabadiliko hayo, Simba ilishindwa kurudi mchezoni, ambapo zikiwa zimebaki dakika nne kabla ya mchezo kumalizika, mwamuzi Ibrahim Kidiwa ‘Mdudu’ alitoa kadi nyekundu kwa Nyoso kwa kumchezea vibaya Barnabas.
Vikosi

Simba: Juma Kaseja, Nasoro Masoud, Amir Maftah, Juma Nyoso, Komanbil Keita, Shomari Kapombe, Ramadhan Chombo/Kigi Makasi, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi/Amri Kiemba na Haruna Chanongo/Mrisho Ngassa.

Mtibwa Sugar: Hussein Shariff, Said Mkopi, Issa Rashid, Salvatory Ntebe, Salum Sued, Shaaban Nditi, Jamal Mnyate, Rashid Gumbo, Hussein Javu, Shaaban Kisiga na Vicent Barnabas.

Source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment