WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Wednesday, December 2, 2015

UTHUBUTU WA RAISI MAGUFULI NA UTUMBUAJI MAJIPU



Katika kipindi chote cha Kampeni Mheshimiwa Dr. Magufuli daima alionyesha upendo, maumivu  na haja ya kuibadilisha Tanzania kuwa kweli ya watanznaia na sio Tanzania ya wachache katika kufurahia matunda yatokanayo na rasilimali la taifa letu. Mfuatiliaji mzuri aliweza kugundua kuwa Magufuli aliamua kwa hiari yake kuwatumikia watanzania kuwa kiongozi mzuri kufuatia kwa ajili ya watanzania wote bila ubaguzi wowote.

Rekodi zake za utendaji kwa falfasa ya kuwa atakuwa kiongozi ambaye  hataficha chochote kwa wananchi; hatasema uongo,  na atafichua uongo kila unapoibuka. hatakuwa mtu wa kuficha matatizo, makosa, mapungufu na kushindwa kuyatafutia suluhu na kamwe sio mtu wa makundi au wa kujijengea sifa nyepesi nyepes binafsi.

Mchakamchaka ambao anaendlea kuufanya Magufuli sasa ndicho haswa kinachotakiwa kufanyika katika kipindi kirefu nyuma. Kwa kufanya hivyo, Magufuli anaonyesha wazi kuwa anajua matatizo na mapungufu yaliyopo na badala ya kuyafunika na kuyapaka rangi anayaweka wazi kwa maendeleo ya watanzania wote. Bahati nzuri Magufuli amekuwa akielezea namna atakavyoshughulikia hayo matatizo na mapungufu. Bahati nzuri tabia hii ya Magufuli siyo mpya. Watanzania watakumbuka kuwa hulka hii ya Magufuli ilijionyesha wakati hata alipokuwa waziri chini ya Rais Benjamin Mkapa alipoikosoa Ofisi yake hadharani kwa baadhi ya watumishi wa ofisi hiyo kujimilikishia magari ya umma isivyo halali. Tukumbuke hata Katika kipindi cha kampeni, Magufuli amekuwa akitoa mapungufu ya serikali hata pale ambapo Rais Kikwete yupo.
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuandika kitabu mwaka 1962 kiitwacho "Tujisahihishe" akitaka Watanzania na hasa viongozi wawe tayari muda wote kujisahihisha. Katika kitabu hicho Baba wa Taifa, alisema kuwa “makosa ni makosa bila kujali ni nani ameyafanya. Muhimu ni kuyajua makosa hayo na kujisahihisha.” Katika kitabu hicho, Mwalimu Nyerere aliendelea kusema;

“Kujielimisha ni kujua ukweli wa mambo na kuwa na ujuzi wa sababu mbalimbali za mambo; na kama mambo hayo ni mabaya ni kujua jinsi ya kuyaondoa; na kama ni mema, jinsi ya kuyadumisha. Mpumbavu ni yule anayeyapa mambo sababu zisizo za kweli na kushauri dawa isiyo ya kweli katika kutafuta sababu za matatizo na jinsi ya kuyaondoa(Nyerere, 1962, 5).”

Kwa maelezo hayo ya Baba wa Taifa, ni wazi kuwa Magufuli ameamua kuwa mkweli katika utendaji wake kama Rais wa wamu ya tano na ameepuka kuwa mpumbavu kama alivyobainisha Baba wa Taifa. Magufuli anaamini dhana hii kiongozi mkweli na aliye na uthubutu wa kujikosoa anaonyesha kuwa ana uwezo wa kutafuta suluhisho la kweli la matatizo yaliyopo, na tumejionea katika kipindi kifupi sana akiwa ameanza kutumbua majipu kama alivyohaidi.



kama mwandishi Maggid alivyowahi andika kuwa Sehemu kubwa ya matatizo ya nchi zetu hizi yanatokana na ubinafsi huo. Na bahati mbaya kabisa, baadhi ya viongozi tuliowapa dhamana za uongozi ndio wenye kuongoza kwa matendo yenye kutanguliza maslahi yao binafsi. Kwetu sisi Watanzania hali yetu ya kiuchumi bado duni mno. Ufisadi unalitafuna taifa letu. Tuna lazima ya kukumbushana ukweli huu, maana, tukifanya masihara taifa letu liko katika hatari ya kuingia katika hali ya machafuko makubwa. Ili kuunusuru uchumi wetu usiyumbe zaidi tuna lazima ya kutumia fedha na rasilimali zetu kwa busara kubwa. Kuna busara ya kutomuiga tembo kwa lolote lile

Sokoine alionyesha moyo wa kujitoa kuwatumikia wananchi mara tu baada ya kuteuliwa katika wadhifa wa waziri mkuu wakati huo akiwa mbunge wa Monduli mkoani Arusha. Katika utawala wake, kama waziri mkuu, aliendesha na kusimamia mwenyewe vita dhidi ya dhuluma iliyokuwa inaendeshwa na wachache wenye nacho dhidi ya wengi wasionacho. Vita dhidi ya walanguzi na wahujumu uchumi ni miongoni mwa mambo ambayo yaliinua jina la Sokoine kila pembe ya nchi hii na katika medani za kisiasa.


Sokoine alipenda haki, aliona ni kitu cha kushangaza kwamba wananchi walio wengi walikuwa wanaishi maisha ya dhiki, hawakusikilizwa na watendaji. Alishangaa kuona kwamba urasimu umezama kwenye rushwa za nipe-nikupe na kuporomoka kwa maadili hasa upungufu mkubwa katika kutoa huduma na haki. Sokoine alitumia uwezo kama waziri mkuu kujaribu kurejesha nidhamu katika sekta ya utawala kwa kuwajibisha viongozi na watendaji wabovu. Kwa upande mwingine, alijitahidi kuvunja ushirikiano kati ya viongozi warasimu na wafanyabiashara ambao kwa pamoja waligeuza sekta ya umma kama shamba la bibi. Hili ndilo analolifanya Magufuli na watendaji wake katika mwezi huu wa kwanza wa awamu yake ya Tano ya kuliongoza Taifa hili.

Dr. Magufuli tuko alipopendekezwa na chama chake cha mapinduzi kupeperusha bendera ya kuwania urais wa awamu ya tano alisema wazi kabisa kuwa wananchi wategemee  utumishi uliotukuka toka kwake, watarajie uadilifu wa khali ya juu,watarajie uchapakazi, watarajie serikali itakayo kuwa imara: itakayo simamia maslahi ya uma; na wategemee nidhamu sio tu kwa watumishi wa serikali bali kwa watanzania wote; wasitegemee propaganda za ujanja ujanja; balo ukweli wakati wote; na alihaidi kufuatilia mambo mengi kwa kina mimi  mwenyewe; wasitarajie sherehe na hafla nyingi toka kwangu. Na watarajie kuwa nitalinda umoja amani na usalama wan chi yetu kwa nguvu yetu zote. Nitakuwa kiongozi wa wote bila kubagua mkoa kanda dini kabila wala vyama.

Kama mwandishi Mmoja alivyowahi andika “Dr John Pombe Magufuli raisi wa awamu ya tano anataka kuwaonyesha watanzania kwa ujumla wake kuwa atakaye aliyethubutu kuchezea shilingi ya Serikali atajitutia yeye mwenyewe; ni kweli ilikuwa inasikitisha kila siku kusoma magazeti yenye vichwa vya habari, Mamilioni yametafunwa yayeyuka na kuunda kamati ambazo zilikuwa vile vile zikitumia pesa katika kutafuta suluhu na suluhu haipatikani. Kama mwandishi Maggid alivyowahi andika  Maana, kuna walioishi wakiamini, kuwa ng'ombe wa Serikali huzikwa na ngozi yake. Ni nani anayejali? Maana, kama ng'ombe ni wa mtu binafsi, basi, akifa, atahakikisha walau anachuna ngozi yake, ili walau aambulie senti kidogo! Utamaduni huu wa kudhibiti mapato ya hazina ni utamaduni mwema utakaomsaidia mwananchi wa kawaida”.


Hatua ambazo ampaka sasa rais Dr Magufuli, ameshchukua ni funzo tosha kwa watu wengine; tunafahamu kuwa kuteuliwa na hatimaye kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa awamu ya tono kulitokana sana na record yake ya uchapakazi, uadilifu, kutoyumbishwa hovyo hovyo kwa sababu ya kusimamia kile anachokiamini kwa manufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla, Hiyo imejidhihirisha zaidi katika wizara zote alizowahi kuziongoza mfano Ujenzi na Miundombinu pamoja na Kilimo na ufugaji. Ni kweli kuwa fundisho tunalopata hapa ni kwamba usingoje mpaka upewe nafasi kubwa ya utumishi ndio uanze kuonyesha namna ya kuwatumikia wananchi.


Dr Magufuli ni visionary leader ambaye anaamini katika jambo moja kuwa mabadiliko ya maisha bora yanawezekana  katika Tanzania yetu. Tatizo ambalo analijua linalokwamisha maisha bora kwa watanzania ni Usimamizi mbovu sekta zote kutokana na ubinafsi, udugu, rushwa. Katika kampeni yake alipotembelea kaburi la hayati sokoine alisifu weledi wa hayati sokoine ambaye alikuwa mkweli, mchukia rushwa, na alikuwa na uthubutu bila kumwogopa kiongozi yeyote Edward Moringe Sokoine alikuwa kiongozi mwenye uthubutu wa dhahiri katika kupigania na hata kufia maslahi ya raia, hasa maskini. Tunamkumbuka Moringe alivyowasha moto  bungeni kabla ya kuondoka, hasa alipozungumza kuhusu kubana matumizi ya serikali, ambako kuliambatana na hoja juu ya ukubwa wa serikali na hasa mantiki ya kuwa na mawaziri wasiokuwa na wizara maalum, lakini wakipatiwa haki zote sawa na mawaziri wenye wizara. Nyota yake ilizidi kung'ara na kuwa chachu ya kupendwa miongoni mwa walio wengi; akaonekana mwiba kwa walafi na wadokozi wa keki ya taifa.  

Ingawa kwa upande mmoja Sokoine alionyesha kupata mafanikio kwa kuungwa mkono na wananchi, kwa upande mwingine alijikuta akipoteza marafiki na kujijengea maadui lukuki kutokana na mfumo wa utendaji uliokuwepo kabla yake. Katika utendaji wake mara zote, Sokoine aliamini katika siasa za uwazi. Alizungumza kile alichoamini ndicho na alisimamia na alionyesha mfano katika utekelezaji wa kila jambo alilotaka lifanyike. Mambo mengi aliyojaribu kufanya Sokoine yalitokana na uthubutu wake binafsi. Alitumia mfano wake kama kiongozi ambaye alikuwa na uadilifu mkubwa na hakuwa na ubinafsi.

Rekodi ya utendaji kazi wa kiongozi huyu ambaye alibahatika kushika wadhifa wa waziri mkuu katika vipindi viwili tofauti, haijafikiwa na kiongozi yeyote katika ngazi hiyo, miongo mitatu tangu kifo chake. Inasemekana ni katika kipindi chake cha uongozi, Mwalimu Nyerere alipata ahueni, alinenepa. 



Na katika awamu hii ya Magufuli watanzania wanyonge ni zamu yao kunenepa; na kuanza kufurahia matunda ya nchi yao tumejionea wenyewe muhimbili wagonjwa wakiwa wamelala katika vitanda na sio katika sakafu.



Kama ilivyokuwa kwa marehemu  Sokoine Mheshimiwa Dr. Magufuli ameanza kuonyesha kuwa atakuwa kiongozi mkuu ambaye ataweza kuisimamia kusimamia serikali kwani ameonyesha kwa moyo mkunjufu kuwa anamainisha kila ambacho anakiongelea na kukiishi. Tunafahamu kuwa viongozi wa aina ya Mwalimu Nyerere na Sokoine hawazaliwi kila mara. Kama taifa tumepata bahati ya ajabu kwani sasa tumempata kiongozi wa aina hii ndio mheshimiwa Dr.John Pombe Joseph Magufuli. Amekuwa kiongozi mwenye ujasiri wa kuchukua maamuzi katika mazingira magumu ambayo yanawagusa hata vigogo wa serikali ili nguvu kubwa zielekezwe kuwasaidia maskini,.


Dr. Magufuri ameonyesha awajibike wa ukweli, kuwa muwazi katika utendaji wake kubana matumizia ya serikali.

Maswali ambayo najiuliza leo

  • Uwajibikaji ulipotelea wapi kwa viongozi wetu?


  • Nini maana ya kuwa kiongozi wa umma?


  •  Je wengi wa viongozi wetu wanaelewa dhana hii nzima ya kuutumikia umma au jamii?


  • Je walioko madarakani na wanaoongozwa wanaonyesha na kufahamu wajibu wao kwa jamii na kuwa viongozi bora wa kuigwa na kizazi chetu cha baadae?


Ninachofurahia mimi katika awamu hii ya tano, misamiati kama kula nchi kwa watendaji wa serikali na mashirika ya umma; dhana ya umungu mtu kwa watendaji wengi sasa inapotea katika kamusi ya utumishi wa umma.


Ni wakati umefika sasa kwa watendaji wetu kujua nini maana ya uongozi; na wakumbuke kuwa uongozi sio maana yake kulindana katika utendaji wa maovu. Imefika wakati wa kuwaambia viongozi wote wabovu umekosea ondoka:  Mheshimiwa Magufuli ameweza kuonyesha hili katika kipindi kifupi sasa cha uongozi wake kama Rais Magufuli ameonyesha kwa dhati Moyo wa kuwatumikia hao waliomchagua na sio kujali maisha yake na familia yake tu kama ambavyo hali ilivyo sasa. Hivi sasa Dr. Magufuli anaifufua dhana yaw a kuwatumikia wanachi ambayo ilikuwa imeshakufa na kupitwa na wakati. Hapa nchini kwetu kila aingiaye madarakani anafikiria kujinufaisha binafsi na waliomzunguka.

Uongozi na kuwa kiongozi Tanzania ilikuwa ni mradi wa kutajirika na wala hakuna anaeuliza mara baada ya kiongozi kuwa madarakani maisha yake kwa ujumla yanabadilika na kuwa ni mtu wa juu kupita wote ndani ya jamii husika. Inashangaza lakini hii ndio hali halisi kwa Tanzania yetu.  Hatukatai mabadiliko lakini hali iliyoko sasa inakatisha tamaa kwa wanaojua maana ya kuwa kiongozi wa umma.

Nimefurahi kwa ujasili wa Dr. Magufuli wa kuondoa  utamaduni uliojengeka wa kusifia makosa na pale mmoja miongoni mwetu anapotaka kusema ukweli huambiwa ni msaliti wakati anachotaka kukisema au alichosema ni cha haki na ukweli kabisa. Asante Mheshimiwa Magufuli kwa kuanza kuibadili dhana hii na kuwabadili na wananchi kwa ujumla huu sio wakati tena wa kuwaachia watu wachache wakitupeleka peleka katika lindi la umasikini na matatizo kutokana na ubinafsi na ulafi wao tu.

Mheshimiwa Magufuli amesema kuwa kazi  iliyo mbele yake ni kubwa na ngumu lakini amekubali kuwa yeye ndiye atakuwa anatumbua haya majipu; hivyo Kama Mwandishi mmoja aliandika kuwa “ Uzalendo wetu kama Watanzania tunaoipenda nchi hii ni kubainisha yale machafu ya viongozi na sio kuwa wanafiki. Ilishasemwa zamani kuwa Ukweli ni mchungu, hatuna budi kuusema japo unauma tuseme ukweli bila ya hivyo matatizo yetu hayawezi kwisha kwa kutegemea wanafiki na walioingia madarakani kwa maslahi binafsi”

Maendeleo ya kweli ya watanzania yatatoka na watanzania wenyewe; Hata siku moja hatotokea mtu toka nje ya nchii hii kuja kutuletea maendeleo ila ni sisi wenyewe tunapaswa kujiletea hayo maendeleo, nayo ni kuwajibika kutokana na dhamana tulizopewa na sio kuipelekea kuzimu nchi yetu kama hali ilivyo sasa. Mfano mdogo tu hebu angalia uozo wa Bandari na TRA na hasara ambayo Taifa limepata.


Mheshimiwa Rais Magufuli ameliona wazi kuwa Kiongozi wa umma anawajibika kwa umma uliomuweka madarakani na sio kufanya safari nyingi za nje na kusema kuwa hana nafasi  na kwenda vivijini kuona shida za watanzania Hongera Dr. Magufuli kwa kuliona hilo. Uamuzi wa hivi karibuni wa  kufuta safari za nje ni wa kishujaa na utapunguza matumizi makubwa ya pesa za wananchi.  Hii inaonyesha jinsi ya ukubwa wa tatizo la viongozi kutowajibika kutokana na nafasi zao ndani ya nchi hii lilivyo.

Ni wakati umefika sasa wa kuanza upya kuanza kujitawala tukaanza kujenga Taifa la viongozi na wananchi wanaowajibika kutokana na nafasi zao kwa maendeleo ya Taifa hili kama ilivyokuwa kwa viongozi waadilifu kama Mwalimu Nyerere na Edward Moringe Sokoine; Unapowajibika kutokana na nafasi ya uongozi inaonesha ni jinsi gani ulivyokuwa kimaadili na kuwa tayari kulitumikia Taifa la wanyonge.




Tukumbuke kuwa zao la viongozi wabovu limezalisha taifa la Watanzania walio wengi sasa wamejikita katika mazingira ya udanganyifu, rushwa na uzembe.  Tukumbuke kuwa Watumishi wa umma wametakiwa kufanya kazi kwa bidii, uwajibikaji, weledi na ushirikiano ili kuuiwezesha Serikali kuwaletea maendeleo wananchi wake na taifa  kwa ujumla. 

MHESHIMIWA RAIS DR. JOHN POMBE MAGUFULI WATANZANIA TUNAKUOMBEA KATIKA SAFARI HII YA UTUMBUAJI MAJIPU KWA AJILI YA MAENDELEO YA WANYONGE: TANZANIA SIO MASIKINI ILA VIONGOZI WACHACHE AMBAO TULIWAKABIDHI NAFASI MBALIMBALI WALIKIUKA MAADILI YA UONGOZI NA KULILETEA TAIFA HASARA KUBWA.

MUNGU IBARIKI TANZANIA MUNGU MBARIKI RAIS WETU MAGUFULI AENDELEE KUWAHUDUMIA WANYONGE NA MASIKINI -TANZANIA







No comments:

Post a Comment