WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, December 28, 2015

MCHANGO WA WAPINZANI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA;


MCHANGO WA WAPINZANI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA;

BADO TUNAHITAJI MCHANGO WA UPINZANI KATIKA KUBORESHA DEMOKRASIA NA UTAWALA BORA NA WA HAKI TUKIZINGATIA KUWA:

  • “Siasa si mchezo mchafu, ila wachezaji wake ndiyo wachafu.”


  • Litakuwa ni jambo la kuheshimiwa ka viongozi wetu wetu watakuwa wakweli na wenye Uzalendo wa kweli ndani ya mioyo kwa faida ya wananchi wao.


  • Confucius aliwahi sema kuwa  ‘Utajiri na vyeo ndivyo vitu ambavyo kila bianadamu anavitamani; lakini ikiwa njia ya kuvipata ni kwa kwenda kinyume na misingi yake, anapaswa ajiepushe navyo.’


  • Rudolph Giuliani aliwahi sema kuwa ‘Kiongozi huchaguliwa kwa kuwa yeyote anayemuweka pale huwa anaamini maamuzi, tabia na uwezo wa maarifa yake – siyo ujuzi wa kufuata maoni. Ni wajibu wa kiongozi kuchukua hatua kufuatana na sifa hizo.’


  • “kiongozi ajiulize ni vipi atalitumikia Taifa na si Taifa kumtumikia yeye Kiongozi Umashuhuri na uzuri wa Kiongozi unatokana na hekima, busara, uchapakazi, ufanisi, ufuatiliaji, uimara, uungwana, uwajibikaji na unyenyekevu wake. Ama fikra endelevu na upeo wa kuongoza ni muhimu na si kauli tamu za kuwafurahisha viongozi wengine”

 

Demokrasia kama falsafa ya Plato ambayo inahusiana na uendeshaji wa shughuli za kisiasa inalenga zaidi katika  utumishi kwa umma na uendeshaji wa jamii na taifa. Wananchi wote hawawezi ongoza nchi kwa mara moja; Katika msingi huu wananchi kutokana na wingi wao waliridhika itakuwa sio rahisi kwa wao wote kukutana, kufanya maamuzi na kuyasimamia moja kwa moja maamuzi hayo yanayowahusu wao kama jamii; dhana ya kuwachagua viongozi wachache huzaliwa kwa chimbuko hili na kuruhusiwa kuunda serikali.


Tatizo kubwa tulilonalo kama Taifa ni ufinyu wa viongozi bora na utashi binafsi wa wachache walio katika nyanja za uongozi kwa kukosa sifa muhimu kwa viongozi. Kwani inatupasa kutambua kuwa uongozi si lelemama, ni kipaji na ni kazi ngumu. Lakini ridhaa hiyo haitolewi hivi hivi tu, inaambatana na amana, kwamba waongozi watatekeleza dhamana  na wajibu  wao kwa makubaliano na maelewano ya kufuata barabara na kuheshimu ipasavyo kanuni na maadili fulani yanayoitambulisha na kuiongoza jamii husika. 


Hapa ndipo chimbuko la demokrasia linapochimbuka na dhana ya Upinzani kwa masilahi ya wananchi linapoanzia. Lengo la vyama nya upinzani ni kuleta ushindani wa kisiasa dhidi ya chama kinachotawala katika nchi husika. Upinzani unasimama kama mbaadala wa wananchi katika kukosoa shughuli za serikali ambazo huzitenda kinyume na utaratibu ambao unafaida kwa taifa husika.


Pamoja na hamu kubwa ya upinzani kushika hatamu lakini husaidia kuleta uwajibikaji na uadilifu kwa viongozi ambao wameshika hatamu ya uongozi. ikumbukwe kuwa kiongozi muadilifu hakubali kufuata  au kutoa maamuzi bila kufanya ukadirifu wa hoja na hali husika. Uongozi ni kujitolea na kuweka matwakwa na maslahi ya wengine kuwa mstari wa mbele na si matakwa binafsi na kujinufaisha.


Marehemu John Kennedy rais wa Marekani alitoa kauli moja maarufu iliyosema kuwa. Tuchague viongozi si kwa kuangalia vyama au sura, bali tuangalie uwezo wao wa kuongoza, kuhamasisha na kufanya kazi. Tupime kauli zao na matokeo ya kazi zao kama wanavyojinadi. Hii ndio dhana ya upinzani inapoingia kwani hutupa sisi wananchi nafasi zaidi ya kupima uwezo wa viongozi kupitia vyama vyao nani unafaa kuongoza nchi kwa kipindi Fulani kulingana na mahitaji ya Taifa.

Tukumbuke kuwa, Serikali ni watu, inaundwa na watu tuliowachagua na tunawapa watu hawa na Serikali mamlaka makubwa ya kutuongoza, kupanga na kulinda Taifa na Katiba yetu. Dhamana hii imefanywa kwa kuaminiana kuwa Serikali itafanya kazi kwa manufaa ya Wananchi wake na kwa matakwa na utashi wa Wananchi wake.


Upinzani tunahitaji ni ule ambao unatija kwa taifa, kwani taifa letu linahitaji utulivu, amani na upendo miongoni mwa wananchi wake na kudumisha umoja wa kitaifa kupitia viongozi wake; kiongozi muadilifu pia hufanya kila bidii kuhakikisha amani na utulivu wa kweli katika nchi vinapatikana. Amani na utulivu ni chachu ya wananchi kwa kushirikiana na Serikali yao kujiletea maendeleo. Maendeleo hayaji mahala penye magomvi na huhasama. Lakini na amani na utulivu pia haviji mahala pasipo na haki na uadilifu. Uvunjifu wa amani na utulivu wa nchi hupelekea hasara ya maisha na mali ya watu na hayo hayawi malengo ya uongozi muadilifu katika nchi wala upinzani wa kweli ambao haujejaa uroho wa madaraka kwa nia binafsi.

Uadilifu wa uongozi unadai kuheshimu nguvu ya hoja na fikra bora na hayo yanaweza kupatikana tu iwapo nchi inaongozwa kwa misingi ya kidemokrasia. Hivyo, katika kutoa uongozi sahihi, kwa kuzingatia maslahi bora ya nchi na watu wake, haki, uadilifu, umoja, amani na utulivu, hapana budi kwa kiongozi kuiamini, kuiheshimu na kuifuata barabara misingi ya kidemokrasia.


Bado binadamu si mkamilifu na kwa vyovyote vile hufikia mahala akafanya maamuzi ambayo si sahihi hata kama yalifanywa kwa nia njema na kwa kuzingatia taarifa zilizopatikana wakati maamuzi hayo yanafanywa. Hayo yanaeleweka na kiongozi muadilifu anapaswa kuyakubali na kuliomba radhi Taifa. Hiki ndiyo kilele na kigezo kikuu cha uadilifu wa uongozi katika siasa. Kukubali kubeba dhamana kwa madhara yaliyotokana na maamuzi yako au yaliyofanywa kwa jina lako.

Maamuzi ya kiongozi wa kisiasa huathiri taifa zima, busara na hekima huzaa maamuzi yanayotokana na tafakuri ya kina, yanayozingatia hali halisi ya mambo na maslahi na manufaa ya muda mrefu. Kiongozi muadilifu anatakiwa ayaone haya na ayazigatie kwa kila hatua anayochukua. Kama viongozi wetu wa bunge wakikiri kuwa walikurupuka katika kufanya maamuzi hayo bila kuyafanyia kazi vizuri heshima na uwajibikaji wa kuliendesha bunge letu itarudi. Tukubali tu kuwa njia ya kusonga mbele ni kukubali kutofautiana katika fikra lakini tubaki kuwa wamoja.


Kama taifa bado tunahitaji upinzani katika uendeshaji wa taifa letu ili kuweza kuikumbusha na kuibana serikali pale ambapo hukiuka utekelezaji wa majukumu yake ya maendeleo kwa wananchi wake; na pale inapokiuka utaratibu wa demokrasia na kukiuka haki za binadamu na matumizi mabaya ya selikali.

Mungu ibarika Tanzania na watu wake.


                           AMEN

No comments:

Post a Comment