WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Tuesday, May 8, 2012

Mawaziri Watoa Ahadi Za Asali Na Maziwa


 MAWAZIRI na manaibu waziri wapya, wameeleza mikakati yao ya kukabiliana na changamoto wakati wa kutekeleza majukumu yao, huku Umoja wa Ulaya (EU), ukiweka bayana kuwa umefurahishwa na mchakato mzima uliomfanya Rais Jakaya Kikwete afanye mabadiliko katika Baraza lake la Mawaziri.

Mawaziri hao walitoa kauli hizo kwa nyakati tofauti jana katika hafla ya kuwaapisha iliyofanyika Ikulu.

EU ambao ni wafadhili katika Mfuko Mkuu wa Bajeti ya Serikali (GBS), umewapongeza wabunge kwa jinsi walivyoibana Serikali bungeni na kumwagia sifa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Ludovick Utouh, kwa kazi nzuri.

Katika mkutano wa Saba wa Bunge, wabunge waliibana Serikali wakitaka iwawajibishe mawaziri wanane ambao wizara zao zilitajwa katika ripoti ya CAG kwamba zilihusika na ufisadi wa fedha za umma hatua ambayo ilimfanya Rais Kikwete kufanya mabadiliko makubwa katika baraza hilo na kuwatupa nje sita.

Mawaziri waliowajibishwa ni William Ngeleja (Nishati na Madini), Dk Hadji Mponda (Afya na Ustawi wa Jamii), Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii), Mustafa Mkulo (Fedha), Dk Cyril Chami (Viwanda na Biashara) na Mhandisi Omary Nundu (Uchukuzi), huku wawili, Profesa Jumanne Maghembe akihamishwa kutoka Kilimo, Chakula na Ushirika na kwenda Maji na George Mkuchika akihamishiwa Ofisi ya Rais, Utawala Bora akitokea Ofisi ya Waziri Mkuu, Tamisemi.
 
Mawaziri walonga

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hussein Mwinyi baada ya kuapishwa alisema atapambana na changamoto zilizopo katika wizara hiyo.

Alizungumzia pia mgomo wa madaktari uliotokea hivi karibuni akisema atafanya kila jitihada kuhakikisha kuwa suala hilo halitokei tena... “Changamoto ni nyingi lakini niwahakikishieni kuwa tutapambana nazo.”

Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe alisema wizara hiyo ina matatizo mengi lakini hawezi kuwa mwarobaini wake bali, atapambana na matatizo hayo ili Uchukuzi iwe ni wizara inayoeleweka na kama ikishindikana atasema.

“Nachukulia kawaida mgawanyo wa kazi, tunaomba muda wa kujua matatizo na kuyarekebisha, tutakuwa tukitoa taarifa,” alisema Dk Mwakyembe.

Alisema vipaumbele ni vingi vya kufanyia kazi akigusia kusimamia Bandari, Reli na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kwamba maeneo yote hayo yanapaswa kufanya kazi kwa ufanisi.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alisema umeme ni kipaumbele muhimu kwake akisema sasa anashangaa kwa nini nchi haina megawati 1,500 za uhakika.

Alisema atahakikisha Watanzania wanapata umeme wa uhakika na kujitahidi kuwa na megawati zipatazo 5,000  ambazo zitasaidia kukuza uchumi na kupunguza makali ya umeme kwa wananchi.

“Mimi siyo mwanasiasa, nimesomea Jiolojia na ninamudu nafasi hii. Haiwezekani hadi sasa ni asilimia 14 tu ya Watanzania ambao wanapata umeme tena usio wa uhakika. Nitakachokifanya ni kuongeza watumiaji wa umeme na kupunguza gharama zilizopo.”

Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda alisema akishirikiana na wizara nyingine atashughulikia tatizo la mfumuko wa bei ambao unaathiri wananchi wenye kipato cha chini. Pia aliahidi kupunguza gharama za ufanyaji biashara na kuondoa urasimu.

“Lazima tupunguze gharama za ufanyaji biashara. Pia tutaangalia yale yaliyozungumzwa bungeni na kuyafanyia kazi,” alisema Dk Kigoda.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki alisema uteuzi wake ni changamoto kubwa akisema ana shaka kwamba wizara anayokwenda ina matatizo lakini akasema lazima wananchi wapate faida ya rasilimali zao na kwa kufanya hivyo ataanzia kwenye ripoti ya CAG  kusafisha njia.

“Watanzania watuangalie utendaji wetu wa kazi. Lazima tuondokane na tabia ya ripoti kuvumbua uovu na kuziacha tu zikapita. Nitahakikisha ripoti ya CAG haipuuzwi. Wizara hii watu wanakula vibaya hivyo nitawashughulikia na haya matatizo ya vitalu na wizi wa nyara za Serikali yote nitayashughulikia.”

Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe alisema Watanzania wategemee Katiba bora ambayo watakuwa wameshiriki kikamilifu kuiandaa... “Tutapokea mawazo ya wananchi kwani ushirikishwaji ndiyo utakaotufikisha.”

Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alisema jambo la kwanza atafuatilia mwenendo wa matumizi ya fedha za Serikali pamoja na kusimamia uwajibikaji kwa watendaji.

Alisema ili aweze kufanikiwa katika hilo, atasimamia vizuri fedha za umma ili zitumike katika shughuli zilizokusudiwa jambo ambalo linaweza kupunguza ufujaji wa fedha za Serikali. Alisema mkakati mwingine ni kuimarisha thamani ya shilingi.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Maselle alisema Watanzania wategemee mabadiliko makubwa katika sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kuwasaidia wachimbaji wadogo ili waweze kuboresha shughuli zao na kuleta tija kwa kundi kubwa la watu.

“Wachimbaji wadogo wanafanya kazi katika mazingira magumu, jambo ambalo limesababisha kuwepo kwa malalamiko ya hapa na pale, mkakati uliopo ni kuweka utaratibu madhubuti ambao utaweza kuwalinda katika shughuli zao,” alisema Masele.

Naibu Waziri wa Habari, Vijana na Utamaduni, Amos Makala alisema Wizara yake ina changamoto nyingi ikiwemo upande wa michezo, hivyo atashirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha kuwa maendeleo ya michezo yanapatikana.

Alisema kutokana na hali hiyo watendaji wake wanafanya kazi kwa ufanisi zaidi jambo ambalo linaweza kusaidia kukuza michezo nchini.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene alisema taifa linakabiliwa na changamoto nyingi hasa za ukosefu wa nishati ya umeme jambo ambalo limesababisha kuwepo kwa malalamiko mengi hivyo kuahidi kushirikiana na wadau kuhakikisha kuwa nishati hiyo inapatikana jambo ambalo linaweza kupunguza adha ya mgawo.

Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba alisema atahakikisha kunakuwa na elimu ya sayansi ili kuzalisha watafiti wazalendo katika masuala mbalimbali akisema elimu hiyo itasaidia pia sekta ya mawasiliano katika nyanja mbalimbali za mawasiliano, sayansi na teknolojia.

“Mkakati wangu ni kuhakikisha kunakuwa na kipaumbele katika tafiti mbalimbali zinazofanywa na taasisi mbalimbali iwe ya elimu ya juu au binafsi ili kuhakikisha kuwa ripoti zake zinafanyiwa kazi.”

Alisema, lengo ni kupiga hatua za kimaendeleo pamoja na kuhakikisha kuwa tafiti hizo zinaleta tija kwa maendeleo ya taifa ikiwa ni pamoja na kuangalia changamoto zilizojitokeza ili ziweze kufanyiwa kazi katika maeneo husika.

Alisema hali hiyo inaweza kufumbua matatizo mbalimbali ambayo Serikali inapaswa kuyarekebisha jambo ambalo litasaidia kukuza uchumi wa nchi na kuleta maendeleo kwa taifa zima.

“Tafiti hizo zitaweza kutoa dira ya uwekezaji katika maeneo mbalimbali nchini jambo ambalo linaweza kuboresha utendaji kwa wafanyakazi na kukabiliana na changamoto za kimaendeleo zinazojitokeza,” alisema.

Kwa upende wake, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja alisema hana kinyongo na hatua iliyochukuliwa na Rais... “Sina kinyongo miaka mitano ya Nishati na Madini si mchezo.”

Mawaziri walioapishwa jana ni Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa), Hussein Mwinyi (Afya na Ustawi wa Jamii), Profesa Jumanne Maghembe (Maji), Hawa Ghasia (Ofisi ya Waziri Mkuu, Tamisemi), Mathias Chikawe( Katiba na Sheria), George Mkuchika (Ofisi ya Rais, Utawala Bora) na Celina Kombani (Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma).

Wengine ni Dk Emmanuel Nchimbi (Mambo ya Ndani), Christopher Chiza (Kilimo, Chakula na Ushirika), Balozi Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii), Dk Harrison Mwakyembe (Uchukuzi), Dk Fenella Mukangala (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo), Dk Abdallah Kigoda (Viwanda na Biashara), Dk William Mgimwa (Fedha) na Profesa Sospeter Muhongo (Nishati na Madini).

Naibu waziri ni Adam Malima (Kilimo, Chakula na Ushirika), Lazaro Nyalandu (Maliasili na Utalii), Gregory Teu (Viwanda na Biashara), Pereira Ame Silima (Mambo ya Ndani), Charles Kitwanga (Ofisi ya Makamu wa Rais), Jerryson Lwenge (Ujenzi), Dk Seif Radhid (Afya na Ustawi wa Jamii), Dk Binilith Mahenge (Maji), George Simbachawene na Steven Maselle wote Nishati na Madini, na Januari Makamba( Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia).

Wengine ni Dk Charles Tizeba (Uchukuzi), Amos Makalla (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo), Angela Kairuki (Sheria na Katiba), Janeth Mbene na Saada Mkuya Salum wote Fedha.

EU yamwaga sifa

Wakizungumzia hatua hiyo, mabalozi wa EU wamesema kubadilishwa kwa mawaziri, ripoti ya CAG na mapendekezo ya wabunge kuhusu ripoti hiyo imeonyesha demokrasia ya kweli kwa Tanzania.

Balozi wa EU nchini, Filiberto Ceriani Sebregondi alisema hayo jana Dar es Salaam wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari baada ya kuzindua wiki ya umoja huo kwa mwaka 2012.

Balozi Sebregondi alisema umoja huo umefurahishwa na mchakato ulivyokwenda kuanzia kwa CAG mpaka mabadiliko ya mawaziri na kusema huko ndiko kuendeleza demokrasia ya kweli.
Alisema kutokana na mabadiliko, watakutana hivi karibuni na kujadili namna ya kusaidia Bajeti ya Serikali ya Tanzania... “Tunafurahi na mabadiliko hayo kwa kuwa yataleta manufaa kwa jamii na hivi karibuni tutakaa na kutangaza kiasi tutakachochangia katika Bajeti ya Tanzania ya mwakani.”

Balozi wa Ujerumani nchini, Klaus Peter Brandes alisema wamefuatilia na kuona majibizano yaliyokuwa yakifanyika bungeni na wamefurahishwa na mazingira aliyowekewa CAG katika kufanya kazi.

“Tumefuatilia na kuona majibizano bungeni, Serikali imefanya vizuri, tunafurahi kwa CAG kufanya alichoagizwa kwa maendeleo ya Tanzania nasi hivi karibuni tutaangalia mataifa yetu tutachangia kiasi gani kwa ajili ya bajeti ijayo,” alisema.

Balozi wa Sweden, Lennarth Hjelmaker alisema: “Tumeona kuwa ripoti ya CAG imeonyesha ukweli na wote tunaunga mkono kilichotokea katika mabadiliko ya mawaziri na mchakato wa bungeni Dodoma.

Habari hii imeandaliwa na Boniface Meena, Festo Polea na Ibrahimu Yamola
 Chanzo; http://www.mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment