WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, March 11, 2012

KAMA TAIFA TUKO WAPI MGOMO WA MADAKATARI




Mgomo Wa Madaktari: Ni Heri Hekima Inayokuja Kwa Kuchelewa... ( Makala Yangu Gazeti Mwananchi, Jumapili)

N

 Ndugu zangu,
Ni heri hekima inayokuja kwa kuchelewa kuliko inayokosekana kabisa.

Maana, ni heri kutibiwa na daktari aliye kazini na moyo mkunjufu kuliko kutibiwa na daktari aliyelazimishwa kwa nguvu kurudi kazini huku akiwa na kinyongo.
Wahenga walinena; unaweza kumlazimisha punda kwenda mtoni, lakini kamwe huwezi kumlazimisha kuyanywa maji. Hilo la mwisho ni la hiyari, kama ilivyo kwa tabasamu, kwamba unaweza kumlazimisha mwanadamu kupiga makofi, lakini kamwe huwezi kumlazimisha kutabasamu, hilo la mwisho latoka moyoni.

Kuna habari za kusikitisha kwa Watanzania, kuwa madaktari wetu wamo tena kwenye mgomo.

Gazeti Mwananchi ( Mtandaoni) linaandika; ” Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana, Waziri Mkuu Pinda, alisema Serikali haioni sababu ya kuwawajibisha mawaziri hao kwa sasa na kueleza kushangazwa kwake na hatua ya madaktari hao kugeuza suala hilo kuwa dai namba moja hivi sasa.

“Hivi kweli mnataka nifike mahali nimwaambie Rais (Jakaya Kikwete) tunakupa saa 72 uwafukuze kazi viongozi hao? Hapana... hapana... hapana kwa lipi hasa? Siwezi kumwambia atekeleze hayo. Ingekuwa hatujafanya chochote sawa, hata angekuwa mtu yeyote hawezi kukubalina na hayo unless (vinginevyo) wenzetu madaktari watuambie wana hoja nyingine.”

Pinda alisema Dk Mponda mwenyewe anayelalamikiwa ndiyo kwanza ana mwaka mmoja na nusu kazini na hata madai mengine hayajui kwa kuwa hakuwepo wakati huo akisema shinikizo la kutaka awajibishwe ni kumuonea.

Alipoulizwa endapo mawaziri hao wataamua kuwajibika wenyewe ili kunusuru maisha ya Watanzania Serikali itakuwa tayari kwa hilo, Pinda alihoji: “Kwa lipi hasa? Naona ni vyema tusubiri majadiliano, hayo yote yatajulikana baada ya kufikia mwisho.”

Waziri Mkuu aliwataka madaktari kutumia busara, hekima na uzalendo na kuendelea na kazi kama kawaida wakati Serikali inaendelea na majadiliano na viongozi wao. ( Mwananchi Mtandaoni, Machi 8, 2012)

Naam, kinachoonekana hapa ni ukweli, kuwa mgogoro wa madaktari na Serikali umeingia katika hatua nyingine mpya. Na hii ni hatua mbaya zaidi, maana, pande zote mbili zinaonekana kujichimbia mahandakini tayari kwa kujipanga kwa vita kubwa zaidi. Vita isiyo na tija.

Huu ni mgogoro na si kitu kingine. Na majeruhi wa kwanza kwenye mgogoro kama huu ni UKWELI. Katika vita yoyote iwayo, risasi ya kwanza huelekezwa kwenye ukweli. Ni hapa ndipo propaganda huchukua nafasi yake. Lakini, kama ni vita, hii itakuwa ni vita ya kiwendawazimu, maana, haitatoa mshindi. Na katika vita hii, sote, kama taifa, tayari tumeshashindwa. Je, tunataka tushindwe mara ngapi?
Tumeona kupitia televisheni jinsi wagonjwa wanavyotahabika kwa kukosa tiba. Kwanini raia wasio na hatia wafe kwa vile watu wazima kwenye pande mbili kwenye mgogoro, zinashindwa kufikia muafaka wa namna ya kwenda mbele? Inasikitisha sana.

Ushauri wa nini kifanyike;

Hatua hii inahitaji busara na hekima zaidi. Walikofikia madaktari kwenye mapambano yao na Serikali haifikiriki kuwa watarudisha’ majeshi’ nyuma. Na walipofikishwa Serikali na madaktari haifikiriki kuwa kuna Waziri au Naibu wake atakayejiuzulu ili kumaliza mgomo. Upande wowote utakaomkubalia mwenzake katika hatua hii utatafsiriwa kuwa umeshindwa.

Na ’position’(nafasi) ya Serikali inachangiwa zaidi na hofu ya ’domino effect.’ Hilo linaeleweka ukiingia kwenye fikra za Serikali. Athari ya ’kidomino’ ina maana ya badiliko moja hata likiwa dogo linapelekea badiliko lingine, na lingine na lingine. Hatma yake ni mparaganyiko wa jumla.

Sasa basi, cha kufanya katika hatua kama hii ni kwa pande mbili kuepuka kuendesha mapambano yao hadharani. Maana, hakuna upande ulio tayari kwa sasa ’ kutua mbanji’ ( kuweka silaha chini) bila kufunika sura (face saving).

Mantiki hapa, ni kuwepo na njia ya tatu; kwamba pande zote mbili ’in a closed door dialogue’( mazungumzo yasiyoruhusu vyombo vya habari kuwepo na hata kutangaza) kufikia makubaliano ya kudumu, ya kimaandishi ya namna ya kwenda mbele; hivyo basi, kwa pamoja, na kupitia taarifa ya pamoja (joint communique) kutangaza muafaka na hivyo ’ kutua mbanji’ huku sura zao zikiwa zimefunikwa.

Kwa mantiki hiyo, wanayohitaji madaktari yafanyike yanaweza yasifanyike kesho , lakini yakaja kufanyika kwa namna nyingine, kwa makubalino kama yasipofanyika, wahusika wa upande mmoja wa kwenye makubaliano wataitaarifu pande nyingine kimaandishi na bila kupitia media, kuwa walichokubaliana kifanyike hakijafanyika na kuwa wamekubaliana kisipofanyika nini kifanyike na ndicho kitakachofanyika.


Na kitapofanyika upande mmoja utakaolalamikiwa juu ya kwanini umefanya walichokifanya, utakuwa na uthibitisho wa kuuleza umma kuwa umefanya ulichofanya kwa vile upande mwingine umekiuka makubaliano ya kimaandishi na umekubaliana nao kimaandishi juu ya hatua waliyoichukua.

Hivyo basi, tulipo sasa, pande mbili kwenye mgogoro huu hazina budi kurudi kwenye meza ya mazungumzo huku wakitanguliza busara, hekima na maslahi mapana ya taifa. Wajifungie na kuanza upya mazungumzo yatakayoleta makubaliano ya kimaandishi.

Wahenga walinena; kwenye wengi hapaharibiki neno. Ni matarajio yetu, kuwa hatma ya mazungumzo kama hayo itakuwa ni kutolewa kwa taarifa ya pamoja kwa umma, na bila shaka itakuwa ni pande zote mbili kukubaliana kwenye mambo ya msingi na kuwa madaktari wanarudi kazini.

Maana, umma wa Watanzania kwa sasa hauna haja ya kuona nani mshindi na nani mshindwa, kwa vile tulipo sasa sote tumeshashindwa. Watanzania hawana haja pia ya kuona nani, leo au kesho , anatundikwa kitanzini na kunyongwa, bali, kuwaona madaktari wao wanarudi kazini na kufanya kazi wakiwa na mioyo mikunjufu.


Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika.
0788 111 765, 0754 678 252  http://mjengwablog.com

No comments:

Post a Comment