WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, February 6, 2012

Uchambuzi Wa Habari: Alichosema Ali Mufuruki



Ndugu zangu,

Kwenye gazeti la Mwananchi jana Jumapili kulikuwa  na habari ukurasa wa tano inayosema; “Mufuruki: Itikadi za kisiaa zinakwamisha wananchi”.  ( Mwananchi Jumapili, Februari 5, 2012)

Habari hiyo ilinivutia sana na ikawa ya kwanza kwangu kuisoma. Mwandishi Exuper Kachenje anaripoti, kuwa  Mwenyekiti wa Jukwaa la Maafisa Watendaji Wakuu wa Kampuni Binafsi nchini  Bw. Ali Mafuruki ametaja kuwa itikadi za kisiasa ni  vikwazo vikubwa  vilivyowanyima  na vinavyoendelea kuwanyima  wafanyabiashara wazalendo nafasi  wakiachwa nyuma  na kuwapendelea  wageni wanaoshikilia uchumi wa Tanzania kwa kiasi kikubwa.

Ali Mufuruki anasema; ” Vikwazo vikubwa kuliko vyote ambavyo mpaka leo vipo ni vile vilivyotokana na itikadi ya kisiasa ambavyo siyo tu ilimnyima nafasi mfanyabiashara mzalendo, bali pia iliwapendelea zaidi wasio wazalendo.”- Ali Mufuruki.

Mufuruki anazidi kubainisha, kuwa kwa muda mrefu Watanzania wengi wenye uwezo wa kufanya biashara kubwa walikimbilia kufanya kazi za kuajiriwa Serikalini, kwenye shughuli za za siasa huku wasio na uwezo  wa kupata ajira  wakihangaika na biashara ndogondogo na kuiacha sekta ya biashara kubwa kwenye mikono ya watu wenye asili ya kiasia.

Bwana Mufuruki akazidi kuwa mkweli na kusema, kuwa waasisi wa Uhuru wetu  walitilia mkazo zaidi udhibiti wa nguvu ya utawala wa kisiasa bila kujali nafasi ya wananchi wao katika kudhibiti nguvu za uchumi. Hilo, kwa mujibu wa Mufuruki, ndilo  lililowaacha  wenye uwezo zaidi kudhibiti nguvu za uchumi wa nchi kwa miaka mingi ijayo.

Mtazamo wangu;

Bwana  Ali Mufuruki amekuja na hoja  ya kizalendo, nzito na muhimu sana kwa nchi yetu kwa sasa. Watanzania tumekuwa kama wagonjwa wa muda mrefu ambao,  waganga mbali mbali  tuliowapata wameshindwa kutwambia chanzo cha maradhi yetu. Hivyo basi, wameishia kujaribisha tiba , moja baada ya nyingine, bila mafanikio. Watanzania bado ni  wagonjwa kiuchumi.

Ali Mufuruki ametusaidia kujua chanzo cha maradhi yetu. Na yuko sahihi kabisa. Alichokisema Mufuruki mara kadhaa nimekiita kuwa ni ubaguzi wa kisiasa. Nchi yetu inasumbuliwa na ’maradhi ya ubaguzi wa kisiasa’. CCM , kama ilivyokuwa kwa TANU, bado inaamini katika udhibiti wa nguvu za kisiasa.

Kuna mifano kadhaa  ya Watanzania wazalendo waliofilisika kibiashara kwa ’ dhambi ya kuwaunga mkono wapinzani’. Tuna mifano kadhaa ya wafanyabiashara Watanzania wenye asili ya kiasia ambao biashara zao zinashamiri kwa vile walichagua tangu enzi, kuwa wafadhili wa TANU na baadae CCM ambayo ina hamu ya kuendelea kudhibiti nguvu za kisiasa badala ya kuandaa mazingira ya wananchi wake wadhibiti uchumi wao.

Wakati CCM ikitimiza miaka 35, hoja ya Ali Mufuruki waichukulie kama changamoto.  Maana, zama za udhibiti wa nguvu za  kisiasa zimepita.  Kwenye pluralism kuna ustawi . Kwenye  ' Chama Kushika Hatamu' kuna kudumaa. Huwezi leo kuendelea na udhibiti wa nguvu za kisiasa kama wananchi wako hawana udhibiti wa nguvu za kiuchumi na badala yake udhibiti huo huko mikononi mwa wananchi wako wachache wenye asili ya kiasia au wageni wanaoitwa wawekezaji.

Na huu si wakati tena wa kuwa na wanasiasa wenye kutoa hadharani, kauli kama; ” Anayetaka biashara yake imwendeee vizuri aje CCM!”

Tubadilike ili tusonge mbele kiuchumi , na tuzidi kuwa Wamoja kama taifa.

Maggid Mjengwa,
Dar es Salaam.
Jumatatu, Februari 6, 2012

Habari kwa Hisani ya Mjengwa Blog

No comments:

Post a Comment