WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, December 14, 2017

KUMBUKUMBU YA MWAKA MMOJA: DARAJA LA UPENDO NA TABASABU LILILOMALIZA KAZI KWA USHINDI:




Leo tunatimiza mwaka mmoja toka mama yetu mpendwa mama Anna kinunda aka Mbuya atangulie mbele ya haki; furaha yetu kubwa ilikuwa jinsi ambavyo aliweza kuipiga vita yake kwa ushindi mkubwa; na kufanikiwa kushinda Tuzo na huku kuendelee kuilinda imani yake mpaka mwisho wa safari yake kama vile Mtume Paulo alivyoandika katika waraka 2 Timotheo 4: 5-8.

Mwaka mmoja unatukumbusha jinsi yeye alivyoyaweka maisha yake katika mwongozo wa Mungu akijua kuwa mapambano ambayo alikuwa akipitia na kuyafanya yalikuwa ni juu yake na Muumba wake na hakuna mtu mwingine yeyote ambaye angeweza kumzuia na kumshawishi tofauti ndio maana aliamini kuwa imani ameilinda: Silaha yake katika ushindi wake ilikuwa ni kutimiza amri kuu ya upendo, ambayo ukiitimiza vizuri utaishi maisha ya uaminifu; hivyo hakukuwa tayari kumpa shetani nafasi kwani aliishi maisha yake ili kumtumikia Mungu na sio maisha ya kujilinganisha na mtu au watu wengine: aliishi vile Mungu alitaka sisi tuishi:

Daima alikuwa akimpendeza Mungu zaidi; na sio kuwafurahisha watu wengine katika mambo ambayo sio ya kimungu; aliishi maisha ya kuwasaida sana wahitaji wale ambao walikuwa wakihitaji msaada; alikuwa tayari kujinyima yeye kwa faida ya taifa la Mungu hasa watoto na wazee ambalo lilikuwa likihitaji msaada; 

Mbuya Anna aliishi maisha ya kutimiza wajibu wake kama mkristo kwa kumpigania Kristo: alitukumbusha wakati wote tusikae chinina kusoneneka na kujilaumu kwa makosa ya jana wajibu wetu daima ni kuomba msamaha na msaada wa Mungu; amakweli Mbuya yeye alichagua fungu lililo sahihi kama Mary katika  Luka 10:41-42 : je wewe na mimi ni akina Martha tunahangaika sana na mambo ya kupita na ya Muda mfupi ya dunia hii?



Tukumbuke kuwa utawala wa Mungu kamwe hautapotea au kufa  kwani juu ya mwamba atalijenaga kanisa lake na hakuna nguvu ya kuzimu ambayo inaweza kulishinda Mathayo 16:18;Mbuya alijua kuwa neema ya Mungu na thamani ya Mungu ilikuwa kuwa zaidi katika maisha yakendio maana aliipigania kwa nguvu zote; je wewe na mimi tunamsimamo gani? Ni wakati wetu sasa wa kusimama imara kumwambia shetani sasa ondoka mbele yangu; umepoteza furaha; upendo wangu; amani yangu na nuru ya uzima wa milele sasa nimesimama na kumwomba anisamehe kwani mimi narudi katika njia iliyo sahihi aipendezayo Mungu; tumwombe Mungu Msamaha kama Daudi alivyofanya katika zaburi ya 51

Tuwe kama Mwana mpotevu aliyetambua makosa yake na kuamua krudi kwa baba na kuomba msamaha wa makosa yake:Mwenyezi Mungu anafurahi pale tunaporudi kwake na kuomba msamaha ili tuweze kushiriki karamu nzuri ya mwana kondoo aliyechinywa kwa ajili yetu;




Raha ya milele mpe bwana na Mwanga wa Milele uendelee kuyangaza maisha yake katika nuru ya Kimungu kwani ameipigana vita vilivyo: Tuzo amepata; na Imani aliilinda na sasa amevikwa Taji lile ambalo alikuwa ameandaliwa pamoja na wale wote ambao wametimiza wajibu wao wa kuishi maisha yaliyompendeza Mungu 

            AMINA                                      AMINA



Tuesday, June 21, 2016

RAISI DR. MAGUFULI NA JICHO JIPYA LA WATENDAJI KATIKA SERIKALI;



Serikali ya awamu ya tano kwa mara ya kwanza imeamua kuwatumia sana wataalamu ambao wana sifa za kielimu katika utendaji wa wake katika idara nyingi serikalini; mwelekeo ambao umekuwa wazi inajitahidi sana kuondoka na kasumba ya kuwapa watu vyeo kwa huluka ya kisiasa kwa kulindana na kurudisha fadhila. Ilikuwa jambo la kawaida hata wasomi wetu kwa sababu ya hulka ya kisiasa hata pale walipokuwa wakipata nafasi za uongozi walikuwa wanazisahau kabisa taalumu zao na kufanya kazi kwa mazoea ya siasa.

kuwa mwana siasa kwa ujumla wake sio  taaluma, ni haki ya kila mtanzania (msomi au sio) lakini lazima tofauti moja iwe bayana kuwa msomi anapongia katika siasa anaangaliwa katika jicho tofauti kwa mategemeo na matarajio kuwa anatafanya kazi kwa weledi mkubwa na kuongeza tija kwa taifa; Kitu ambacho kwa kipindi kirefu kilikuwa sio kweli. Ilikuwa ni aibu na hasara ambayo Tanzania imekuwa ikipata kwa wasomi wake kujiingiza katika siasa ambazo mchango wake kwa maendeleo ya taifa ulikuwa ni mdogo kuliko angejikita katika kufanya utafiti unaohusiana na fani yake.
Kwa wasomi wetu kuingia katika siasa ilikuwa ni mwanzo wa kuzika taaluma zao; hata pale ambapo walitakiwa kutoa ushauri ambao ungekuwa na manufaa makunwa kwa taifa, hata kama ushauri huo ungekuwa mchungu kwa serikali mara nyingi walikuwa wakitoa ushauri wenye masilahi kwa mtu au chama. Hivyo kuwa hasara kwa Taifa. Kwa wakati huo ilikuwa vyema kwa  Siasa kuwaachie wanasiasa.

Mara nyingi tumechambua kuwa siasa ni mchezo mchafu; lakini ukweli ni kuwa siasa kama mfumo hauna tatizo lolote, wenye tatizo ni wachezaji wanasiasa ambao moja ya sifa yo kubwa ni uwezo wa kuongea na kubadilisha maneno ili sio kuwasaidia wananchi ili kujinufaisha kupitia chama Fulani na uundwaji wa serikali yao; hivyo hata wasomi wetu kama raia wa Tanzania hakuna tatizo kama hao wasomi wanajiingiza kwenye siasa. Shida ni pale wanapokuwa wanasiasa waongo na wasioaminika.

Inatakiwa tufike mahali kama ilivyo kwenye nchi za mataifa yaliyoendelea kuwa utagundua wanasiasa ni wanasiasa na wataalamu huwa hawajichanganyi kwani muda wote wako wakiumiza vichwa kufikiria jinsi ya kugundua kitu fulani. Linapokuja tatizo katika jamii huwa wana wanajitahidi kutimiza wajibu wao kwa kutumia utaalamu wao katika kuleta suluhu ya tatizo.

Tunamshukuru Dr. Magufuli kwa kuanza kutaka kupata matokeo chanya kutoka kwa wasomi wetu katika awamu hii wamepewa mafasi kubwa ili weweze sasa kufanya kazi kwa utaalamu na sifa ambazo wanazo kwa faida ya Taifa na kuwaondolea wananchi wa kawaida ugumu wa maisha ambo uko mbele yao; ni kweli ilikuwa jambo la  aibu sana kuona hadi hii leo Serikali imeshindwa kutumia wasomi wake na rasilimali zilizopo kuleta ufanisi katika kuleta maendeleo kwa wananchi wake matokeo yake ni usanii wa kisiasa ndio uliowekwa mbele. Lakini kubwa zaidi ni kuona hata pale inapopatikana fursa ya ukombozi kujikwamua katika ujinga na umaskini wa kujitakia,hutokea Wasomi wetu kutusambaratisha wenyewe kwa wenyewe.

Wasomi wetu awamu hii ni kipindi chenu cha kuumiza na kushauri na kubuni mipango ya kuwafanya Watanzania katika kuleta mageuzi makubwa ya uchumi na maisha ya watu wake; Dr. Magufuli  anategemea sana ushauri na misimamo madhubuti ya wasomi ili kuisadia serikali katika kujenga Tanzania Mpya. Katika siku za nyuma ilikuwa sahihi kusema kuwa  wananchi wa nchi hii walikuwa na  shahada ambazo zilikuwa hazitumiki zilikuwa zimefungiwa kwani nafasi zao zilichukuliwa na wanasiasa ambao walikuwa hawana sifa za utendaji kwa Taalumu bali kwa siasa; Tumeona mifano ya Maprofesa wengi wasio na idadi, wengi amboa walikuwa wamekijikita kwenye siasa hivyo taaluma yao ilikuwa haina nafasi ili walazimu kucheza ngoma ya siasa na sio ngoma ya utaalamu wao katika kutoa ushauri au kutekeleza adhima ambayo ilikuwa mbele yao.

Katika mazingira yetu, tunapozungumzia Siasa, watendaji wote walilazimika kuwa chini ya mwamvuli wa maagizo ya chama na serikali yake na si vinginevyo hivyo walitakiwa kukizi zaidi zaidi matakwa na mahitaji ya watawala kuliko matakwa na mahitaji ya jamii. Ni jambo la kawaida kwa vyama vya siasa kutumia muda mchache sana kujishughulisha na matatizo/changamoto zinazokabili jamii na badala yake kujikita katika masuala yanayohusiana na uongozi na kutwaa madaraka. Lakini Mheshimiwa Dr. Magufuli anataka wasomi wetu ndio sana wawe chachu ya utawala Bora; wawe ni chimbuko la ufanisi na utatuzi wa Migogoro; wawe ndio daraja bora la maendeleo kwa taifa kwa kutumia uwezo wao wa  kuchanganua, kutambua, na kuelewa jambo. Na na ndio maana wasomi  katika jamii yoyote ile wana uwezo mkubwa wa kuona masuala mbali mbali zaidi ya mwanasiasa wa kawaida kwa  maslahi mapana ya kitaifa.

Tofauti na miaka ya nyuma, Tanzania ya leo imejaliwa kuwa na wasomi wengi sana waliotokana na vyuo vyetu vikuu. Vyuo vikuu ni taasisi zenye umuhimu wa kipekee wa kupangilia na kuendeleza kitu amhacho jamii inaweza kuakisi. Lakini kwa vile wasomi wana nafasi na uwezo wa kushughulika na masuala mbalimbali ya kijamii hawa ndio wenye jukumu kubwa la kuisaidia jamii yetu iondokane na umaskini ambao kwa mshangao mkubwa na bila aibu

kama kioo cha jamii – kwa maana ya kwamba inaipa jamii taswira yake. Wasomi wa nyanja mbali mbali wana uwezo na wajibu wa kutuelezea watanzania tunaonekana vipi kama jamii. Wasomi wana uwezo na wajibu pia kutupa tahadhari juu ya hatari iliyopo mbele yetu; na vile vile kutusaidia kutupatia maana ya vitu ambavyo wanasiasa wetu aidha wanavipotosha, hawavielewi au wanafanyia mzaa kwa faida zao binafsi. Na kwa mara nyingine nina imani kuwa katika awamu hii ile dhana iliyojengeka na jamii yetu ya kuamini wanasiasa na kuliko wasomi ina weza sasa ikapata tafsiri tofauti. 

Lakini ni wajibu wa wasomi wetu kuidhihirishia jamii kuwa wao ndio watatuzi wa kero zetu na sio wansiasa ambao walio wengi hawana taaluma inayotakiwa katika kupambana na kero tofauti tofauti.

Tukumbuke wakati wa Mwalimu alivyoweza kuwatumia wasomi wetu kwani miaka ya 1960s – 1970s, kila wakati taifa lilipokuwa linakabiliwa na changamoto mbalimbali, Mwalimu alikuwa na utamaduni wa kwenda Chuo Kikuu (Mlimani) kukutana na kujadiliana na wanafunzi. Ndio maana tofauti na leo, ilikuwa ni mara chache sana kwa serikali ya Mwalimu kukwaruzana na wasomi. Ni muhimu kwa wasomi kuendeleza juhudi za aina hii.Lengo kubwa Raisi Dr. Magufuli ni kujenge upya dhana ya utendaji kazi yenye nidhamu, uwajibikaji na weledi kwa Taifa na kuondoa utendaji kazi wa mazoea. Sasa ni wakti umefika kwa wasomi wetu ambao mmepewa dhamana ya kuongoza vitengo mbali mbali kulingana na taaluma zetu kufanya kazi katika msingi huo wa utendaji ambao utakuwa na tija kwa taifa letuna faida ya wananchi wetu na mageuzi ya kweli ya uchumi wa Taifa letu;
Mungu Ibariki Tanzania: 

Mungu Mbariki Raisi wetu na dhamira yake nzuri ambayo ameanza kuionyesha kwa Taifa.

Amina

Tuesday, April 5, 2016

SERIKALI ZENYE RUSHWA NA UFISADI – KIINI CHAKE NI NINI?



Wafilipi 2: 4


Leo tujitafakari  na tujiulize kuwa je kuna serikali yeyote ya kidunia ambayo inaweza kuwa madarakani bila kuwa na kutumikia rushwa na ufisadi? Tukumbuke kuwa mwisho wa siku watumishi wa serikali bado ni raia wa nchi husika na zao la taifa husika; Je kwa mantiki hii viongozi ambao wanaunda serikali wanaweza kuepukana na vitendo vya rushwa na ufisadi? Je unakubaliana nami kuwa serikali za kidunia zimejaa rushwa na ufisadi ambao ni ubatili mtupu? Je tunaweza kuwa na serikali ambayo haina tabia hizi katika dunia hii? Bibilia inatukumbusha kuwa  serikali ambayo haitakuwa na harufu ya rushwa lazima itoke nje ya serilaki za kibinadamu;

Tafakari ya leo inatukumbusha kuwa serikali za kidunia ambazo hatimaye zinatawaliwa kwa rushwa na ufisadi, zinasaidiwa kuingia madarakani na raia ambao wanakuwa na malengo tofauti kwa masilahi yao binafsi; wengine wakijua wazi kuwa endapo serikali hiyo itaingia madarakani basi haja zao za kukwepa ushuru, au kuendesha biashara yao bila kufuata masilahi mapana ya nchi yatafanikiwa; hivyo na serikali itatengeneza mianya ya wao kuendelea kujinufaisha na kuwaacha wananchi wanyonge masikini katika umasikini wao kwani nguvu nyingi zitaelekezwa kwao. Tumeona sehemu kubwa za tawala hizi watu ambao ni waaminifu ndio wanaoumia zaidi.

Tafakari ya leo inatukumbusha kuwa ili tuweze kuangamiza rushwa na ufisadi lazima nguvu za kutokomeza zianzie kwa viongozi wa juu ambao wamepewa mamlaka juu ya nchi na Mwenyezi Mungu. Serikali yeyote ile ambayo itakuwa tayari kupambana na rushwa na ufisadi ujue kuwa itapoteza umaarufu wake; katika hili bibilia tukisoma Mhuburi 7:20 bila shaka hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani, ambaye afanya mema, asifanye dhambi.

Tafakari yetu bado inatuongoza kuwa  tukiondoa wanadamu ambao sio wakamilifu; Yesu Kristo ambaye Mungu alimchagua kutawala ufalme wake, hakuweza kushawishika katika yale ambayo yalikuwa sio sahihi kutenda;  Yesu alionyesha hili pale alipokataa rushwa  kubwa ambazo alipewa na shetani juu ya kukabidhiwa utawala wote wa kinunia na fahari zake kwa kuambiwa kumsujudia shetani Mathayo 4: 8-10  kisha ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha miliki zote za ulimwengu na fahari yake; akamwambia haya yote nitakupa , ukianguka kunisujudia; Ndipo Yesu akamwambia Nenda zako shetani, kwa maana uimeandikwa msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. Katika shida na mateso yote bado Yesu aliendelea kudumisha msimamo wake ulio sahihi wa kumtumikia Mungu bila kushawishiwa na mtu mwingine yeyote kwa ukombozi wetu sisi.

Ni ukweli mtupu kuwa nchi nyingi zinafanya uchaguzi ambao nadharia inaruhusu watu kuwachagua viongozi ambao wataingia ofisini/madarakani kwa ajili ya kuendesha nchi; lakini ukiangalia chaguzi nyingi na taratibu za chaguzi hizo hizo ambazo tunaona kampeni zake  nanatawaliwa kwa rushwa kwa kiasi kikubwa sana, hivyo wale wenye uwezo ndio wanaowaingiza watawala madarakani; hapa nafikiri utakubaliana na mimi vyama vya siasa ndivyo vinavyoongoza kwa matendo makubwa sana ya rushwa katika kuhakisha kuwa viongozi tukona vyama vyao ndio wanakuwa washindi ili waweze kuongoza serikali, hivyo watafanya kila hila ili waweze kushinda.

Tafakari yetu ya leo inawaasa viongozi wetu kuwa ili kuweza kuepukana na tabia zote za rushwa na kifisadi; lazima watekeleze amri kuu ya upendo ambayo ni amri ya dhahabu; kile ambacho wewe unataka ufanyiwe mfanyie mwenzako hivyo hivyo; Mathayo 7:12 Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu; nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hili kwa viongozi wetu wengi ambao ndio tegemeo la kuondoa umasikini wa watu wao wameshindwa kutekeleza hili; wao wanapenda kutendewa vizuri na kundi dogo la watu waliowaingiza madarakani na kunufaishana wao kwa wao; wameshindwa kabisa kutekeleza hii Golden Rule.

Kwa msingi huu rushwa na ufisadi unaimarishwa zaidi na choyo ya mali na ubinafsi wa kujililbikizia mali; hapa tunaona kuwa viongozi wako tayari kupokea rushwa mfano kutoka kwa makandarasi, nao makandarasi wanapata nafasi ya mwanya wa rushwa katika kutumia vifaa ambavyo havina ubora unaotakiwa ili waweze kujilipa na kupata faida kubwa; kwa msingi huu rushwa na ufisadi utaweza tu kwisha kama tutaondoka na dhana ya ubinafsi na choyo ya kujitajirisha; kama Waefeso 4:23 inavyotufundisha na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu: tunatakiwa kuvua uongo na tunatakiwa kusema kweli daima ili tuweze kuvaa utu mpya ulioumbwa katika mungu ili kutekeleza wajibu wetu ipasavyo na kuwa na hofu ya Mungu. Na ujumbe huu kutoka katika waraka wa Paulo kwa Wafilipi 2:4  ni muhimu sana ambapo anatufundishwa kuwa Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe bali kila mtu aangalie mambo yaw engine.

Tatizo la tawala za kiduani hata kama wakati mwinginwe wanaweza patiwa elimu nzuri ya kupambana na rushwa na ufisadi bado viongozi wetu wanapenda kushiriki katika vitendo vya rushwa. Kwa msingi huu ni vigumu kwa serikali zetu kupambana na rushwa; tukumbuke mafundisho ya bibilia kuwa watu wenye uchu wa mali, na waongo hawataingia mbinguni; mara nyingi viongozi wala rushwa wana hizi tabia mbili ya Uchoyo wa mali na uongo wanapowadanganya watu wake ili kuhalalisha uovu wao na kikundi kidogo kilicho waingiza madarakani kwa masilahi yao;

Hii ndio tafakari yetu ya leo Amina

Emmanuel Turuka
Corrupt Government


.


Wednesday, March 9, 2016

MIEZI MINNE YA DR. JOHN POMBE MAGUFULI NA TANZANIA MPYA:-

 

JE FALSAFA YA MHESHIMIWA MAGUFULI YA HAPA NI KAZI TU NI SAWA NA  SEMI HIZI?

Kumpa mtu samaki utakuwa umemlisha katika siku ya leo; ukiweza  Kumfundisha mtu  namna ya kuvua samaki  utakuwa umeweza kumsaidia kumlisha katika maisha yake yote.

Ukiweza kumfundisha mtu namna ya kutengeneza na kusafirisha na kuweza kuuza samaki katika masoko ya nje; utakuwa umefanikiwa kuchochea maendeleo ya kiuchumi

Raisi Magufuli toka aliposhika nafasi ya kuliongoza Taifa la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ameendelea kuwa gumzo la utendaji uliotukuka hasa akipigania maendeleo ya wananchi Masikini. Amekuwa na maono ya  uzalendo wake kwa kujitoa kwa kusimamia vizuri rasilimalia za taifa letu. Ameweza kuonyesha umahili katika kusimamia nidhamu ya utendaji katika Wizara na idara zote za serikali, huku akibana matumizi ili kuelekeza nguvu zaidi katika miradi ya maendeleo ambayo inawagusa wananchi moja kwa moja.

Raisi magufuli katika kipindi hiki kifupi amweza kujijengea sifa ya kuwa "unforgettable" miongoni mwa viongozi wa juu wa Tanzania na amekuwa kipenzi cha wanyonge ambao wanamwona kama mkombozi wao katika shida na umasikini wao. Mfano maauzi yake ya haraka ya kuwanusuru wagonjwa waliokuwa wanalala chini katika hospitali zetu; vitendo kama hivyo wananchi wananwmona Dr. Magufuli kama Kiongozi mwenye  maono ya   maendeleo ya nchi yake:

Katika kipindi hiki kifupi ameweza kusimamia ukusanyaji wa mapato ya serikali ambayo yameongezeka sana na kusaidia katika kupunguza utengemezi hasa katika bajeti ya maendeleo ambayo tulikuwa tunategemea sana ufadhili na kukwamisha shughuli za msingi za maendeleo ya Taifa letu. Amekuwa kiongozi ambaye ameonyesha uwezo wa Kujenga na kuboresha uchumi, wetu katika siku zijazo mbele; Ameweza pia kukuza mifumo ya kiutawala na sera zinazolenga zaidi katika kusimamia maisha na ukuaji wa uchumi wa nchi ili tuweze kuondokana na tatizo kubwa la umasikini wa Taifa letu.

Nimejaribu kueleza hayo yote ili kuonyesha kuwa bila kuwa na uongozi wenye maono usiotafuta faida yake wenyewe, usiokuwa tayari kuwawajibisha watendaji wabovu na wanaokiuka maadili na uvunja sheria  hatuwezi kutoka hapa tulipo, tutaendelea kufurahia kauli mbiu ambazo hazina maana wala msingi mkubwa kwa maendeleo ya Taifa.

Kwa sasa Taifa linamwitaji kiongozi mwadilifu, mkweli ambaye anaweza kupambana na matatizo ya rushwa na ufisadi bila kuyaonea aibu. Ili kulivusha Taifa la Tanzania katika mabadiliko ya maendeleo ambayo kama taifa tunayahitaji kwa sasa; tunahitaji Kiongozi ambaye anauchungu sana na nchi yake hasa katika kuwasaidia wananchi ambao ni wanyonge ambao wanahitaji mkate wao wa kila siku na watoto wao waweze kwenda shule; Tumeliona hili kwa Raisi wetu Dr. Magufuli amekuwa msimamizi wa khali ya juu wa utekelezaji wa mpango wa mabadiliko ambayo kama taifa tunayahitaji kwa sasa; katika kampeni alituhahidi kuwa  hana mchezo hata kidogo katika hili  na hatakuwa na msamaha kwa wale wote ambao hawatafikia malengo ambayo serikali yake imeainisha kutekeleza.

Ameshatoa onyo kwa viongozi na wafanyakazi kuwa hayuko tayari kuona kuwa rasilimali ya taifa zinachezewa na wajanja wachache, ikibainika serikali yake itawafukuza kazi bila huruma;  Kwa Dr, Magufuli  ufanisi utakuwa unapimwa kwa uwajibikaji na uadilifu na sio propaganda za kisiasa.

Mheshimiwa Magufuli amepania kurudisha kwenye kamusi maneno uwajibikaji na uwajibishaji kwa watendaji wa serikali katika taasisi zake na idara zake,  na ameamua kuondoa kabisa kwenye kamusi maneno kama utashi wa kisiasa urafiki na undugu na michakato katika kutekeleza wajibu katika majukumu yako ya kikazi.

Mheshimiwa Magufuli anaamini kuwa  hakuna maendeleo ya kweli kama tutaendelea kuendekeza utashi wa kisiasa; ni dhahiri kuwa tuwe tayari kuhesabu kuwa hakuna maendeleo ya haraka yatapatika katika nchi yetu bado tukiwa tunatawala na michezo michafu ya siasa; tukumbuke kuwa majukumu  ya kiserikali yanatakiwa kuzingatia zaidi, misingi yake ya utendaji, na utaalamu, nidhamu na ukweli na sio kuendekeza  urafiki na undugu. 

Mheshimiwa Magufuli amethubutu na amejitangazia wazi kuwa yeye ni sadaka ya watanzania katika kupambana na ufisadi na yuko tayari kujitoa Muhanga ili tu watanznaia wanyonge waweze kunufaika na rasilimali za taifa lao.

Mheshimiwa Magufuli utendaji wake unaongozwa na kauli mbiu ya sitawaangusha: Hapa Ni Kazi Tu; katika imani kuwa ameona umasikini na tabu ya Taifa letu hivyo kama watanznia walivyojenga imani kwake hivyo naye ameweka juhudi zote katika kusimamia kwa dhati kabisa rasilimali za Taifa ili kurudisha matumaini makubwa kwa serikali yake anayoiongoza kwa wananchi kwa maendeleo yao.

Binafsi kama mtanzania na mfuatiliaaji wa utendaji wa kazi  Dr. John Pombe   Magufuri,   pamoja  na  mapungufu yake kama binadamu amekuwa miongoni mwa viongozi wachache ;   kama  kiongozi wa juu kabisa hataki kuona watendaji ambao wako chini yake wanatenda kazi kwa mazoea; daima ameonyesha kuthubutu katika kutekeleza sheria na kuwashugulikia watendaji wabovu  huku akiwa tayari kufuata sheria na kujielimisha ili aweze kuzielewa zaidi sheria  za nchi na wizara husika;  

kwa keli ni ni msimamiaji mzuri  wa sheria katika utendaji hata  kama  wakati  mwingine  maamuzi yake yanakuwa kero kwa kwa watendaji wenzake wanaomzunguka lakini bado yanafaida kubwa kwa jamii ya Kitanzania. Kimsingi    kama  nilivyoainisha  hapo  juu  inawezekana  magufuli  akawa  na  madhaifu  yake  lakini  huwezi  kuondoa ukweli kuwa katika kipindi hiki kifupi cha uongozi wake amekuwa kiongozi mzuri wa Juu aliyeweza kufanya  vizuri katika kazi ya kusimamia hata kuchukua hatua kali kwa wakati dhidi ya wale wote ambao wamekuwa na hawafuati maadili ya kazi na vinara wote wa Rushwa na Ufisadi. Hilo  hata     wananchi   wa  kawaida  wameliona hilo nao wamempa tano.

Ni ukweli  ni wazi  kuwa  Magufuli ni kiongozi mchapakazi  na msimamizi mzuri  “Mnyonge mnyongeni  lakini  haki yake mpeni, wengi tunamtambua Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya, tunakuomba uendelee kufanya hivyo hivyo na  Serikali yake ya awamu ya tano iendelee kujiepusha kufanya kazi na watendaji wabovu:  

Watanzania wamemchagua mheshimiwa Magufuli kwa sababu utendaji wake kazi mzuri na kuwa kiongozi ambaye ameonyesha kiwango cha juu cha maadili; na ameonyesha katika kampeni zake kuwa yuko tayari kuwavusha wananchi  kuelekea katika bandari ya salama na yenye amani na maisha bora.

Magufuli ameonyesha upendo wa juu kabisa sio tu kwa watanzania wote bila kujali itikadi zao au dini zao au makabila yao. Ni kiongozi ambaye anaonyesha  upendo kwa wananchi wote; kwake uongozi ni kwa ajili ya wote na sio watu wachahce tu.

Tukumbuke kuwa kuwa uongozi ni dhana nzito ya kuaminiwa ambayo unakabiziwa na watu; lakini na kwa  kuwa uongozi wa kweli ni matokeo ya kuwa na maadili mazuri. Tukumbuke kuwa kuweza kutekeleza majukumu yako vizuri, Lazima kuwe na uhuisano wa karibu kati ya uongozi na mwongozo.
 
Mheshimiwa Magufuli tunaweza sema kuwa  amejitambua mwenyewe kuwa kazi moja ambayo anakabiliwa nayo ni kuwaletea mabadiliko wananchi wa Tanzania hivyo amejiaamini YeYe mwenywe kuwa anaweza kufanya hivyo hivyo anayo mizizi ya huruma na uvumilivu ndani  na ni mtu ambaye haogopi kushindwa

Kiongozi bora atahangaika kuhakikisha kuwa maisha ya wananchi wake yanasonga mbele na kuwa na misha bora. Ukiwa mnyonyaji wewe ni kiongozi mbovu; viongozi ni viashiria vya mabadiliko katika jamii, na kuendeleza mafanikio tukumbuke kuwa sio vigumu kumtawala mtu ila jukumu ni kumwendeleza mtu.

Viongozi wanaishi kwa kuelewa mazingira na tabia za watu; kiongozi lazima awe tayari kuyapokea mabadiliko kila kitu kinaendelea kubadilika; kiongozi lazima ajue kuwa haitakiwi kuogopa awe tayari kujifunza na kamwe ahitimu shule ya mabadiliko, kiongozi lazima awe tayari kuishi na mabadiliko ya tamaduni. kiongozi mzuri anajua mapungufu ya watu wake, mapungufu yetu yanakamilishwa na wengine ambao wanautaalamu zaidi.

uvumilivu ni nguzo muhimu kwa viongozi wazuri ( role model). kiongozi mzuri lazima ajue kuwa kushindwa ni sehemu ya uongozi bora kwani inakupa nguvu ya kuanza upya, unawapenda watu wako kama huwapendi basi usiwe kiongozi hata kama watu hawakupendi bali kama kiongozi bado unatakiwa kuwajali.

kiongozi lazima ujifunze kutokuona wivu wa mafanikio ya watu wengine sio kukosoa kila kitu hata kama mwenzako amefanya vitu vizuri tabia ya kupongezana ni nzuri sana kwa kiongozi mwenzake. viongozi ni wabunifu ambao wanatakiwa kuleta mabadiliko na kuleta utamaduni wa kazi na kudumisha utamaduni wa mafanikio ni wajibu wa kiongozi mzuri, kwa hiyo viongozi wanatakiwa kuwa viashiria wa mabadiliko ya kweli kwa taifa.

 
kiongozi wanatakiwa kuwa na mawazo mazuri ya kimaendeleo na kujua namna ya kuyatumia kwa ajili ya maendeleo ya watu wao na kwa faida ya watu wao, mgonagano wa mawazo ni sehemu tu ya uongozai mzuri. kiongozi hatakiwi kuhangaika wakati kunatokea matatizo ndani ya uongozi kila kitu kipo kwenye mpito. kiongozi lazima uelewe kuwa yale uliyojifunza shuleni wakati mwingine hayafnayi kazi wakati wote na tayari kufahamu kuwa kufanyia utafiti mabadiliko ya tamaduni za uongozi wako.

VIVA MAGUFULI TUNAKUJUA WEWE NI:

Ni Jembe:
Ni Tingatinga
Ni Mtumishi wa watanzania wote
Unayajua mapungufu yako.
Unaongoza kwa usemi wa sisi sisi.
Ni Mnyenyekevu na mtumishi wa watu wote.
Ni mwadilifu
Mtu wa watu hasa wanyonge
Ni Mwogopa Mungu

VIVA MHESHIMIWA  JOHN POMBE MAGUFULI RAISI WA AWAMU YA TANO MWENYEZI MUNGU AKUPE NGUVU YA KULIVUSHA SALAMA TAIFA LA TANZANIA KATIKA MIAKA HII MITANO KATIKA MAENDELEO AMBAYO  SISI WATANZANIA TUMEYASUBIRI KWA MIAKA MINGI SANA;

UKADIRIFU INAKUTAKIA UONGOZI BORA MIEZI HII MINNE YA UONGOZI WAKO KAMA RAISI WA AWAMU YA TANO


Monday, December 28, 2015

MCHANGO WA WAPINZANI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA;


MCHANGO WA WAPINZANI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA;

BADO TUNAHITAJI MCHANGO WA UPINZANI KATIKA KUBORESHA DEMOKRASIA NA UTAWALA BORA NA WA HAKI TUKIZINGATIA KUWA:

  • “Siasa si mchezo mchafu, ila wachezaji wake ndiyo wachafu.”


  • Litakuwa ni jambo la kuheshimiwa ka viongozi wetu wetu watakuwa wakweli na wenye Uzalendo wa kweli ndani ya mioyo kwa faida ya wananchi wao.


  • Confucius aliwahi sema kuwa  ‘Utajiri na vyeo ndivyo vitu ambavyo kila bianadamu anavitamani; lakini ikiwa njia ya kuvipata ni kwa kwenda kinyume na misingi yake, anapaswa ajiepushe navyo.’


  • Rudolph Giuliani aliwahi sema kuwa ‘Kiongozi huchaguliwa kwa kuwa yeyote anayemuweka pale huwa anaamini maamuzi, tabia na uwezo wa maarifa yake – siyo ujuzi wa kufuata maoni. Ni wajibu wa kiongozi kuchukua hatua kufuatana na sifa hizo.’


  • “kiongozi ajiulize ni vipi atalitumikia Taifa na si Taifa kumtumikia yeye Kiongozi Umashuhuri na uzuri wa Kiongozi unatokana na hekima, busara, uchapakazi, ufanisi, ufuatiliaji, uimara, uungwana, uwajibikaji na unyenyekevu wake. Ama fikra endelevu na upeo wa kuongoza ni muhimu na si kauli tamu za kuwafurahisha viongozi wengine”

 

Demokrasia kama falsafa ya Plato ambayo inahusiana na uendeshaji wa shughuli za kisiasa inalenga zaidi katika  utumishi kwa umma na uendeshaji wa jamii na taifa. Wananchi wote hawawezi ongoza nchi kwa mara moja; Katika msingi huu wananchi kutokana na wingi wao waliridhika itakuwa sio rahisi kwa wao wote kukutana, kufanya maamuzi na kuyasimamia moja kwa moja maamuzi hayo yanayowahusu wao kama jamii; dhana ya kuwachagua viongozi wachache huzaliwa kwa chimbuko hili na kuruhusiwa kuunda serikali.


Tatizo kubwa tulilonalo kama Taifa ni ufinyu wa viongozi bora na utashi binafsi wa wachache walio katika nyanja za uongozi kwa kukosa sifa muhimu kwa viongozi. Kwani inatupasa kutambua kuwa uongozi si lelemama, ni kipaji na ni kazi ngumu. Lakini ridhaa hiyo haitolewi hivi hivi tu, inaambatana na amana, kwamba waongozi watatekeleza dhamana  na wajibu  wao kwa makubaliano na maelewano ya kufuata barabara na kuheshimu ipasavyo kanuni na maadili fulani yanayoitambulisha na kuiongoza jamii husika. 


Hapa ndipo chimbuko la demokrasia linapochimbuka na dhana ya Upinzani kwa masilahi ya wananchi linapoanzia. Lengo la vyama nya upinzani ni kuleta ushindani wa kisiasa dhidi ya chama kinachotawala katika nchi husika. Upinzani unasimama kama mbaadala wa wananchi katika kukosoa shughuli za serikali ambazo huzitenda kinyume na utaratibu ambao unafaida kwa taifa husika.


Pamoja na hamu kubwa ya upinzani kushika hatamu lakini husaidia kuleta uwajibikaji na uadilifu kwa viongozi ambao wameshika hatamu ya uongozi. ikumbukwe kuwa kiongozi muadilifu hakubali kufuata  au kutoa maamuzi bila kufanya ukadirifu wa hoja na hali husika. Uongozi ni kujitolea na kuweka matwakwa na maslahi ya wengine kuwa mstari wa mbele na si matakwa binafsi na kujinufaisha.


Marehemu John Kennedy rais wa Marekani alitoa kauli moja maarufu iliyosema kuwa. Tuchague viongozi si kwa kuangalia vyama au sura, bali tuangalie uwezo wao wa kuongoza, kuhamasisha na kufanya kazi. Tupime kauli zao na matokeo ya kazi zao kama wanavyojinadi. Hii ndio dhana ya upinzani inapoingia kwani hutupa sisi wananchi nafasi zaidi ya kupima uwezo wa viongozi kupitia vyama vyao nani unafaa kuongoza nchi kwa kipindi Fulani kulingana na mahitaji ya Taifa.

Tukumbuke kuwa, Serikali ni watu, inaundwa na watu tuliowachagua na tunawapa watu hawa na Serikali mamlaka makubwa ya kutuongoza, kupanga na kulinda Taifa na Katiba yetu. Dhamana hii imefanywa kwa kuaminiana kuwa Serikali itafanya kazi kwa manufaa ya Wananchi wake na kwa matakwa na utashi wa Wananchi wake.


Upinzani tunahitaji ni ule ambao unatija kwa taifa, kwani taifa letu linahitaji utulivu, amani na upendo miongoni mwa wananchi wake na kudumisha umoja wa kitaifa kupitia viongozi wake; kiongozi muadilifu pia hufanya kila bidii kuhakikisha amani na utulivu wa kweli katika nchi vinapatikana. Amani na utulivu ni chachu ya wananchi kwa kushirikiana na Serikali yao kujiletea maendeleo. Maendeleo hayaji mahala penye magomvi na huhasama. Lakini na amani na utulivu pia haviji mahala pasipo na haki na uadilifu. Uvunjifu wa amani na utulivu wa nchi hupelekea hasara ya maisha na mali ya watu na hayo hayawi malengo ya uongozi muadilifu katika nchi wala upinzani wa kweli ambao haujejaa uroho wa madaraka kwa nia binafsi.

Uadilifu wa uongozi unadai kuheshimu nguvu ya hoja na fikra bora na hayo yanaweza kupatikana tu iwapo nchi inaongozwa kwa misingi ya kidemokrasia. Hivyo, katika kutoa uongozi sahihi, kwa kuzingatia maslahi bora ya nchi na watu wake, haki, uadilifu, umoja, amani na utulivu, hapana budi kwa kiongozi kuiamini, kuiheshimu na kuifuata barabara misingi ya kidemokrasia.


Bado binadamu si mkamilifu na kwa vyovyote vile hufikia mahala akafanya maamuzi ambayo si sahihi hata kama yalifanywa kwa nia njema na kwa kuzingatia taarifa zilizopatikana wakati maamuzi hayo yanafanywa. Hayo yanaeleweka na kiongozi muadilifu anapaswa kuyakubali na kuliomba radhi Taifa. Hiki ndiyo kilele na kigezo kikuu cha uadilifu wa uongozi katika siasa. Kukubali kubeba dhamana kwa madhara yaliyotokana na maamuzi yako au yaliyofanywa kwa jina lako.

Maamuzi ya kiongozi wa kisiasa huathiri taifa zima, busara na hekima huzaa maamuzi yanayotokana na tafakuri ya kina, yanayozingatia hali halisi ya mambo na maslahi na manufaa ya muda mrefu. Kiongozi muadilifu anatakiwa ayaone haya na ayazigatie kwa kila hatua anayochukua. Kama viongozi wetu wa bunge wakikiri kuwa walikurupuka katika kufanya maamuzi hayo bila kuyafanyia kazi vizuri heshima na uwajibikaji wa kuliendesha bunge letu itarudi. Tukubali tu kuwa njia ya kusonga mbele ni kukubali kutofautiana katika fikra lakini tubaki kuwa wamoja.


Kama taifa bado tunahitaji upinzani katika uendeshaji wa taifa letu ili kuweza kuikumbusha na kuibana serikali pale ambapo hukiuka utekelezaji wa majukumu yake ya maendeleo kwa wananchi wake; na pale inapokiuka utaratibu wa demokrasia na kukiuka haki za binadamu na matumizi mabaya ya selikali.

Mungu ibarika Tanzania na watu wake.


                           AMEN

Friday, December 25, 2015

NGUVU YA UTUMBUAJI MAJIPU NA FALSAFA YA MPE KAISARI YALIO YA KAISARI:



Swali la msingi ambalo najiuliza sana hivi sasa hii dhana ya utumbuaji wa majipu ambao umelipatia sana hasara taifa letu asili yake wapi na kwa nini tumefikia hapa ambapo tumefika leo hii kama taifa tukiwa tumepoteza mapato mengi sana ya taifa kwa muda mrefu na taifa kukosa mwelekeo.

Jambo la msingi ambalo halipingiki ni kuwa viongozi wa taifa letu ambao walipewa dhamana ya kutuongoza walikuwa wakitekeleza dhana ya uongozi bora kwa tafsiri binafsi. Dhana ya uongozi inatakiwa ianzie wapi?

Dhana ya uongozi wa namna yeyote ile unafaa uanzie nyumbani kwa kila mtu  uongozi ni uwezo wa kuweza kuyakabili kwanza matatizo  yako mwenyewe na kufanya maamuzi sahihi bila kushawishiwa na mtu mwingine yeyote yule.

kwa kufanya hivyo utakuwa umefanikiwa kuyatawala maisha yako kulingana utaratibu ambao wewe mwenyewe umejiwekea kuanzia ndani ya familia yako;  ukifanikiwa hili unakuwa umefaulu katika mtihani huu wa kwanza wa uongozi ndipo jamii inapoanza kukuona kuwa hata ukipata nafasi ya  kuwaongoza wao pia utaweza kufanya maamuzi sahihi. 

 Kwa maneno mengine ni uwezo au njia ya kuweza kuwashawishi watu ili waweze kufanya kitu au kufikia lengo fulani la kikundi kwa ridhaa yao wenyewe. ili uongozi uwe bora ni lazima kuwe na kiongozi anayeongoza kundi fulani la watu au jamii husika kwa usahihi na kufuata maaadili ya uongozi yanayozingatia uaminifu, ukweli na uadilifu.

Katika kila jamii kuna umuhimu wa kuwa na kiongozi kunatokana na ukweli kwamba watu wanapaswa kuwa na namna ya kuunganisha nguvu zao ili kufikia malengo yao. Katika  kila jamii, ni lazima kuwepo na mikakati ya kuunganisha nguvu, vipaji, uwezo na stadi mbalimbali za wana jamii. 

Wajibu wa msingi wa kiongozi yoyote ni kusaidia kuunganisha uwezo wa watu, kuratibu, kusimamia shughuli za watu, na kila inapobidi aonyeshe njia itakayosaidia kufikia lengo. Hii ndio dhana ya serikali ya awamu ya tano chini ya Dr. John Magufuli ambaye ameonyesha utayari wa kufanya kazi na viongozi ambao wataonyesha uadilifu katika kazi zao za kuwatumikia watanzania ili kuwakwamua  kutoka katika wimbi la umasikini na kuwawajibisha viongozi wote wabadhilifu ambao wamehujumu uchumi wa watanzania.

Kwa dhana ya Plato uongozi ni dhana  au taaluma inayompa muhusika madaraka na uwezo wa kuwawezesha wale wanaoongozwa kuunganisha nguvu, stadi na vipaji vyao na kuvitumia ili kufikia malengo ya Taifa lao ili kujikwamua kutoka katika tabaka kandamizi ambalo linawasumbua. Kuongoza ni kujua lengo la wale wanaoongozwa na njia ya kufikia lengo lao.

Uongozi bora una mchango mkubwa sana katika uimara wa jamii. Lakini tufahamu kuwa Ubora wa kiongozi unachangiwa na vitu vingi lakini tusisahau kuwa vile vile uongozi au kiongozi bora hutoka kwa Mungu. Kama rais wa awamu ya tano alivyowahi sema kuwa serikali yake ina kazi na dhamana nzito wa kuwajengea uchumi wa kati jamii ya watanzania kwa kuelewa kuwa  wakiwatendea watanzania ndivyo sivyo adhabu yao itatoka pande mbili kwa Mungu na kwa jamii iliyowachagua.

Ikumbukwe kuwa viongozi wetu waelewe kuwa ni viongozi muhimu sana ambao wataingia katika vitabu vya kumbukumbu ya Taifa hili kuhusu ubora au ubaya kwa Taifa letu.  

swali la kuwauliza Viongozi wetu wa awamu ya tano Je watendaji wake watampa Kaisari yaliyo ya Kaisari  ili kutimiza yale waliokuwa wamehaidi wakati wa kampeni ili kubadilisha maisha ya watanzania?

Je Viongozi wa awamu ya Tano chini ya mwitikio wa Hapa Kazi Tu chini ya DR. Magufuli   wanafahamu ukubwa na umuhimu wa maamuzi yao kwa jamii ya Tanzania?

Je viongozi wetu wa awamu ya tano  wametawaliwa na maadili gani katika utendaji wa kazi yaokuendesha serikali? Ni ukweli usio fichika kuwa ili waweze kufanikiwa katika kutumiza maendeleo ya wananchi
ni lazima wazingatia maadili ya msingi ya kufanikisha  na kusimamia kwa weledi mkubwa falfasa ya Mpe kaizari yaliyo ya kaizari hasa katika kipengele ya ukusanyaji kodi ili kuimalisha mfuko wa serikali kwa maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Rais Dr Magufuli ameonyesha nia dhabiti katika kutekeleza falfasa hii kwa kuanza kutumbua majipu na kupaisha makusanyo ya kodi katika mwezi huu wa December 2015. Kama taifa tunafarijika kuwa timu nzima ya serikali kwa nia nzuri sasa wanawajibika na kuwawajibisha wale wote ambao walikuwa wanakwenda kinyume na falfasa hii ambayo Yesu aliwambia wafarisayo kuhusu dhana ya kutoa kodi.

Tunaendelea kufarijika kila siku njisi watendaji wakuu wa serikali wanavyowajibika sasa na kuruduisha imani kwa Watanzania masikini kuhusu mabadiliko ya maisha yao na jamii nzima. Hivyo ni vyema waendelee kutimiza wajibu badala ya kujali maslahi yao binafsi yatokanayo na itikadi au faida ambayo wanafikiria wao tu watanufaika nayo na sio taifa;

Daima Rais wetu ameendelee kusisitiza kuwa Tanzania niyetu sote na rasilimali ambazo tumejaliwa ni zetu sote na sio mali ya kikundi Fulani tu. Na ameendelea kusisitiza kuwa  anafafahamu wananchi wanatamani nini; wanatamani watoto wao wapate elimu bora ndio maana sasa serikali imerudisha tena elimu bure kwa watoto wetu;

Anajua watanzania wanataka umoja  ndio maana anaendelea kuhubiri na kuwaomba  wananchi kuendelea kudumisha amani iliyopo katika pande zote mbili za jamuhuri ya Muungano;

Hebu tujikumbushe Busara za Baba wetu wa Taifa  Mwalimu Nyerere alipozungumzia dhana ya uongozi, Mwalimu Nyerere alisema, “uongozi ni kuonyesha njia.” Kwa maana hiyo, viongozi shurti wafahamu vyema matokeo ya uongozi wao. Wasome imani za wanaowaongoza na nyakati zilizopo ili kutambua matumaini ya umma kimaisha.

VIONGOZI GANI TUNAWAHITAJI?

Amabao hawawezi jisahau wamepewa dhamana ya  kushika hatamu ya uongozi la msingi hapa ni kuwa kiongozi amabye yuko tayari kuongoza na  na ajuwe anabeba jukumu la kubadilisha hali za watu kuwa nzuri. Atumie stadi za uongozi mwema kuonyesha njia. Mheshimiwa Dr. Magufuli ameweza kulionyesha hili kuwa kiongozi ambaye anajali Taifa na sio kukitumikia kikundi Fulani.

Wanaepuka kutumia stadi za uongozi kusimamia haki za waliowa wafikisha hapo hasa wanyonge. Wajikumbushe kuwa kupewa uongozi ni kuchukua ahadi ya kutenda kwa haki. Ukitaka kulitendea haki jipu lazima ulikamue na ulikamue vizuri na kuhakikisha kuwa kiini kimetoka ili kumpa nafuu mgonjwa. Ugonjwa ambao kama taifa tunao kwa sasa ni uchumi wetu ambao hauendani na maisha ya wananishi wetu. Tunashkukuru majipu haya sasa yanaendelea kutumbuliwa na mgojwa wetu uchumi anaendelea kuimarika.


Mwalimu Nyerere aliandika miongozo mizuri katika Azimio la Arusha miongoni mwao  akisema kwamba ili tuendelee tunahitaji Siasa Safi na Uongozi Bora. Alitambua mchango wa mambo hayo katika maendeleo ya mwanadamu. Kupitia siasa safi kila kitu cha kunufaisha wananchi hupatikana. Bali ni muhimu viongozi wanaotarajiwa kufanikisha ustawi wa wanadamu, wapatikane kwa njia ya haki. Watokane na ridhaa ya watu wenyewe wanaotaka kuongozwa. Na wakisha chaguliwa anatende kazi kwa uadilifu na ustadi mkubwa. Waweze kukusimai uchumi wetu kwa kuhakikisha kuwa yaliyo ya Kaizari anapewa Kaizari kwa faida ya Taifa nzaima.


Watendaji wetu timizeni wajibu wenu ili muweze kumsaidia rais wetu katika kufanikisha adhima ya kulijenga taifa letu kiuchumi kwa faiada ya vizazi vyetu

Mungu ibariki Tanzania