WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, December 31, 2015

BAADHI YA MATUKIO YALIYO TIKISA TAIFA KATIKA MWAKA 2015



mwaka 2015 kama taifa tumeshuhudia ajali nyingi sana zikiendelea kudhoofisha uchumi wa taifa letu kwa kuwapoteza watanzania wenzetu wengi ambao wamefarika katika ajali zilizosababishwa na ajali nyingi za barabarani kama makala ya hapo juu ilivyoelezea. umekuwa mwaka wa huzuni kubwa kwani kuna baadhi ya ajali tungeweza kuzizuia kama wahusika wangekuwa makini.




Katka mwaka wa 2015 Mheshimiwa Zitto aliaga rasmi kuachana na chama cha CHADEMA; lilikuwa ni tukio ambalo liligusa nyoyo za wapenzi wengi wa siasa wale wa upinzani na wa chama tawala pia.



Katika Mwaka huu wa 2015 Mheshimiwa Lowassa alikihama chama cha mapinduzi na kujiunga na chama cha Upinzani CHADEMA ili kuweza kuwania kugombea urais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.



DR. John Pombe Magufuli aliteuliwa na chama chake ili kuogombea nafasi ya Urais wa Jamuhuri ya Muungano ya Tanzania, kitu ambacho hakikutarajiwa na wengi, kutoka kuwa hakuwa na makundi ndani ya chama hicho , uwajibikaji wake uadilifu wake ndivyo vilimfikisha hapo alipofika.



Katka Mwaka wa 2015 tulishuhudia Prof Ibrahim Lipumba akiamua kuacha na siasa kama mwenyekiti wa CUF na Mwenyekiti Pacha wa UKAWA, kwa kuto ridhika na taratibu ndani ya UKAWA katika harakati za kumpata mgombea urais kupitia muungano huo.


Dr Slaa pia katika mwaka huu wa 2015 aliamua kuachana na siasa akiwa kama katibu mkuu wa CHADEMA. hilo lilitoka na tofauti zilizojitokeza ndani ya UKAWA. lilikuwa ni tukio lililovuta hisia za wengi.



Tukio nyingine kubwa katika mwaka wa 2015 ni CCM kushinda uchaguzi Mkuu uliofanyika October 2015 ; ambapo mgombea wa urais wa CCM Dr. JPM na Makamu wa Kwanza Mwanamke katika historia ya Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan walikabidhiwa vyeti vya ushindi.



DR. JPM awashukuru wana CCM kwa kumchagua na kuanza kuwasha cheche kuhusu unafiki wa baadhi ya wanachama wa chama hicho


Tumeshuhudia Rais DR. JPM akianza kazi kwa ujasili wa kuwa tayari kutumbua majipu ambayo yamerudisha sana nyuma maendeleo ya watanzania.

katika mwaka huu 2015 tuliona wananchi kuguswa na hotuma ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania alipofungua Bunge la 11 kwani ilikuwa imegusa kiu yao na matarajio yao ya muda mrefu. ilikuwa hotuba ambayo imeonyesha mwelekeo wa serikali yake kwa kipindi cha miaka 5 ya utumishi wake kwa umma wa watanzania hasa wanyonge.


Ilikuwa shangwe na vigelegele wakati DR.JPM alivyofanya ziara za kushitukiza na kugundua jinsi watanzania walivyokuwa wakikosa hudumu muhimu kwa uzembe wa wa watendaji, hivyo Katibu Mkuu Kiongozi alitoa mchumuisho wa ziara ya Mheshimiwa Rais na majumuisho ya uwajibikaji kwa wazembe.


Katika mwaka huu wa 2015 Waziri Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa alifanya ziara ya Ghafla Bandarini Na TRA na kujionea njinsi Taifa lilivyokuwa likipoteza kiasi kukubwa cha mapato kwa Tamaa ya watendaji wachacche ambao walikuwa hawana maadili.  ziara hiyo iliweza kubadilisha ukusanyaji wa mapato na serikali kuanza kupata mapato mengi zaidi.


Katika mwaka wa 2015 tumeshuhudia jinsi Rais Dr. JPM akishiriki kufanya usafi wa mazingira. Lilikuwa ni tukio ambalo liliweza kumjumuisha kila mtu kushiriki kufanya usafi ikiwa na sehemu ya kusherekea siku ya kumbukumbu ya uhuru wa nchi yetu.

Tunawatakieni sherehe njema za kuaga mwaka 2015 na kuukaribisha mwaka mpya wa 2016 kwa amani na utulivu na tuendelee kumwombea Rais wetu ili katika mwaka huu wa 2016 aendelee kutekeleza majuku yake, kwa kasi kwa faida ya watanzania kama alivyoanza. Mwenyezi Mungu amjalie afya njema  Amen
.

Monday, December 28, 2015

MCHANGO WA WAPINZANI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA;


MCHANGO WA WAPINZANI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA;

BADO TUNAHITAJI MCHANGO WA UPINZANI KATIKA KUBORESHA DEMOKRASIA NA UTAWALA BORA NA WA HAKI TUKIZINGATIA KUWA:

  • “Siasa si mchezo mchafu, ila wachezaji wake ndiyo wachafu.”


  • Litakuwa ni jambo la kuheshimiwa ka viongozi wetu wetu watakuwa wakweli na wenye Uzalendo wa kweli ndani ya mioyo kwa faida ya wananchi wao.


  • Confucius aliwahi sema kuwa  ‘Utajiri na vyeo ndivyo vitu ambavyo kila bianadamu anavitamani; lakini ikiwa njia ya kuvipata ni kwa kwenda kinyume na misingi yake, anapaswa ajiepushe navyo.’


  • Rudolph Giuliani aliwahi sema kuwa ‘Kiongozi huchaguliwa kwa kuwa yeyote anayemuweka pale huwa anaamini maamuzi, tabia na uwezo wa maarifa yake – siyo ujuzi wa kufuata maoni. Ni wajibu wa kiongozi kuchukua hatua kufuatana na sifa hizo.’


  • “kiongozi ajiulize ni vipi atalitumikia Taifa na si Taifa kumtumikia yeye Kiongozi Umashuhuri na uzuri wa Kiongozi unatokana na hekima, busara, uchapakazi, ufanisi, ufuatiliaji, uimara, uungwana, uwajibikaji na unyenyekevu wake. Ama fikra endelevu na upeo wa kuongoza ni muhimu na si kauli tamu za kuwafurahisha viongozi wengine”

 

Demokrasia kama falsafa ya Plato ambayo inahusiana na uendeshaji wa shughuli za kisiasa inalenga zaidi katika  utumishi kwa umma na uendeshaji wa jamii na taifa. Wananchi wote hawawezi ongoza nchi kwa mara moja; Katika msingi huu wananchi kutokana na wingi wao waliridhika itakuwa sio rahisi kwa wao wote kukutana, kufanya maamuzi na kuyasimamia moja kwa moja maamuzi hayo yanayowahusu wao kama jamii; dhana ya kuwachagua viongozi wachache huzaliwa kwa chimbuko hili na kuruhusiwa kuunda serikali.


Tatizo kubwa tulilonalo kama Taifa ni ufinyu wa viongozi bora na utashi binafsi wa wachache walio katika nyanja za uongozi kwa kukosa sifa muhimu kwa viongozi. Kwani inatupasa kutambua kuwa uongozi si lelemama, ni kipaji na ni kazi ngumu. Lakini ridhaa hiyo haitolewi hivi hivi tu, inaambatana na amana, kwamba waongozi watatekeleza dhamana  na wajibu  wao kwa makubaliano na maelewano ya kufuata barabara na kuheshimu ipasavyo kanuni na maadili fulani yanayoitambulisha na kuiongoza jamii husika. 


Hapa ndipo chimbuko la demokrasia linapochimbuka na dhana ya Upinzani kwa masilahi ya wananchi linapoanzia. Lengo la vyama nya upinzani ni kuleta ushindani wa kisiasa dhidi ya chama kinachotawala katika nchi husika. Upinzani unasimama kama mbaadala wa wananchi katika kukosoa shughuli za serikali ambazo huzitenda kinyume na utaratibu ambao unafaida kwa taifa husika.


Pamoja na hamu kubwa ya upinzani kushika hatamu lakini husaidia kuleta uwajibikaji na uadilifu kwa viongozi ambao wameshika hatamu ya uongozi. ikumbukwe kuwa kiongozi muadilifu hakubali kufuata  au kutoa maamuzi bila kufanya ukadirifu wa hoja na hali husika. Uongozi ni kujitolea na kuweka matwakwa na maslahi ya wengine kuwa mstari wa mbele na si matakwa binafsi na kujinufaisha.


Marehemu John Kennedy rais wa Marekani alitoa kauli moja maarufu iliyosema kuwa. Tuchague viongozi si kwa kuangalia vyama au sura, bali tuangalie uwezo wao wa kuongoza, kuhamasisha na kufanya kazi. Tupime kauli zao na matokeo ya kazi zao kama wanavyojinadi. Hii ndio dhana ya upinzani inapoingia kwani hutupa sisi wananchi nafasi zaidi ya kupima uwezo wa viongozi kupitia vyama vyao nani unafaa kuongoza nchi kwa kipindi Fulani kulingana na mahitaji ya Taifa.

Tukumbuke kuwa, Serikali ni watu, inaundwa na watu tuliowachagua na tunawapa watu hawa na Serikali mamlaka makubwa ya kutuongoza, kupanga na kulinda Taifa na Katiba yetu. Dhamana hii imefanywa kwa kuaminiana kuwa Serikali itafanya kazi kwa manufaa ya Wananchi wake na kwa matakwa na utashi wa Wananchi wake.


Upinzani tunahitaji ni ule ambao unatija kwa taifa, kwani taifa letu linahitaji utulivu, amani na upendo miongoni mwa wananchi wake na kudumisha umoja wa kitaifa kupitia viongozi wake; kiongozi muadilifu pia hufanya kila bidii kuhakikisha amani na utulivu wa kweli katika nchi vinapatikana. Amani na utulivu ni chachu ya wananchi kwa kushirikiana na Serikali yao kujiletea maendeleo. Maendeleo hayaji mahala penye magomvi na huhasama. Lakini na amani na utulivu pia haviji mahala pasipo na haki na uadilifu. Uvunjifu wa amani na utulivu wa nchi hupelekea hasara ya maisha na mali ya watu na hayo hayawi malengo ya uongozi muadilifu katika nchi wala upinzani wa kweli ambao haujejaa uroho wa madaraka kwa nia binafsi.

Uadilifu wa uongozi unadai kuheshimu nguvu ya hoja na fikra bora na hayo yanaweza kupatikana tu iwapo nchi inaongozwa kwa misingi ya kidemokrasia. Hivyo, katika kutoa uongozi sahihi, kwa kuzingatia maslahi bora ya nchi na watu wake, haki, uadilifu, umoja, amani na utulivu, hapana budi kwa kiongozi kuiamini, kuiheshimu na kuifuata barabara misingi ya kidemokrasia.


Bado binadamu si mkamilifu na kwa vyovyote vile hufikia mahala akafanya maamuzi ambayo si sahihi hata kama yalifanywa kwa nia njema na kwa kuzingatia taarifa zilizopatikana wakati maamuzi hayo yanafanywa. Hayo yanaeleweka na kiongozi muadilifu anapaswa kuyakubali na kuliomba radhi Taifa. Hiki ndiyo kilele na kigezo kikuu cha uadilifu wa uongozi katika siasa. Kukubali kubeba dhamana kwa madhara yaliyotokana na maamuzi yako au yaliyofanywa kwa jina lako.

Maamuzi ya kiongozi wa kisiasa huathiri taifa zima, busara na hekima huzaa maamuzi yanayotokana na tafakuri ya kina, yanayozingatia hali halisi ya mambo na maslahi na manufaa ya muda mrefu. Kiongozi muadilifu anatakiwa ayaone haya na ayazigatie kwa kila hatua anayochukua. Kama viongozi wetu wa bunge wakikiri kuwa walikurupuka katika kufanya maamuzi hayo bila kuyafanyia kazi vizuri heshima na uwajibikaji wa kuliendesha bunge letu itarudi. Tukubali tu kuwa njia ya kusonga mbele ni kukubali kutofautiana katika fikra lakini tubaki kuwa wamoja.


Kama taifa bado tunahitaji upinzani katika uendeshaji wa taifa letu ili kuweza kuikumbusha na kuibana serikali pale ambapo hukiuka utekelezaji wa majukumu yake ya maendeleo kwa wananchi wake; na pale inapokiuka utaratibu wa demokrasia na kukiuka haki za binadamu na matumizi mabaya ya selikali.

Mungu ibarika Tanzania na watu wake.


                           AMEN

Friday, December 25, 2015

NGUVU YA UTUMBUAJI MAJIPU NA FALSAFA YA MPE KAISARI YALIO YA KAISARI:



Swali la msingi ambalo najiuliza sana hivi sasa hii dhana ya utumbuaji wa majipu ambao umelipatia sana hasara taifa letu asili yake wapi na kwa nini tumefikia hapa ambapo tumefika leo hii kama taifa tukiwa tumepoteza mapato mengi sana ya taifa kwa muda mrefu na taifa kukosa mwelekeo.

Jambo la msingi ambalo halipingiki ni kuwa viongozi wa taifa letu ambao walipewa dhamana ya kutuongoza walikuwa wakitekeleza dhana ya uongozi bora kwa tafsiri binafsi. Dhana ya uongozi inatakiwa ianzie wapi?

Dhana ya uongozi wa namna yeyote ile unafaa uanzie nyumbani kwa kila mtu  uongozi ni uwezo wa kuweza kuyakabili kwanza matatizo  yako mwenyewe na kufanya maamuzi sahihi bila kushawishiwa na mtu mwingine yeyote yule.

kwa kufanya hivyo utakuwa umefanikiwa kuyatawala maisha yako kulingana utaratibu ambao wewe mwenyewe umejiwekea kuanzia ndani ya familia yako;  ukifanikiwa hili unakuwa umefaulu katika mtihani huu wa kwanza wa uongozi ndipo jamii inapoanza kukuona kuwa hata ukipata nafasi ya  kuwaongoza wao pia utaweza kufanya maamuzi sahihi. 

 Kwa maneno mengine ni uwezo au njia ya kuweza kuwashawishi watu ili waweze kufanya kitu au kufikia lengo fulani la kikundi kwa ridhaa yao wenyewe. ili uongozi uwe bora ni lazima kuwe na kiongozi anayeongoza kundi fulani la watu au jamii husika kwa usahihi na kufuata maaadili ya uongozi yanayozingatia uaminifu, ukweli na uadilifu.

Katika kila jamii kuna umuhimu wa kuwa na kiongozi kunatokana na ukweli kwamba watu wanapaswa kuwa na namna ya kuunganisha nguvu zao ili kufikia malengo yao. Katika  kila jamii, ni lazima kuwepo na mikakati ya kuunganisha nguvu, vipaji, uwezo na stadi mbalimbali za wana jamii. 

Wajibu wa msingi wa kiongozi yoyote ni kusaidia kuunganisha uwezo wa watu, kuratibu, kusimamia shughuli za watu, na kila inapobidi aonyeshe njia itakayosaidia kufikia lengo. Hii ndio dhana ya serikali ya awamu ya tano chini ya Dr. John Magufuli ambaye ameonyesha utayari wa kufanya kazi na viongozi ambao wataonyesha uadilifu katika kazi zao za kuwatumikia watanzania ili kuwakwamua  kutoka katika wimbi la umasikini na kuwawajibisha viongozi wote wabadhilifu ambao wamehujumu uchumi wa watanzania.

Kwa dhana ya Plato uongozi ni dhana  au taaluma inayompa muhusika madaraka na uwezo wa kuwawezesha wale wanaoongozwa kuunganisha nguvu, stadi na vipaji vyao na kuvitumia ili kufikia malengo ya Taifa lao ili kujikwamua kutoka katika tabaka kandamizi ambalo linawasumbua. Kuongoza ni kujua lengo la wale wanaoongozwa na njia ya kufikia lengo lao.

Uongozi bora una mchango mkubwa sana katika uimara wa jamii. Lakini tufahamu kuwa Ubora wa kiongozi unachangiwa na vitu vingi lakini tusisahau kuwa vile vile uongozi au kiongozi bora hutoka kwa Mungu. Kama rais wa awamu ya tano alivyowahi sema kuwa serikali yake ina kazi na dhamana nzito wa kuwajengea uchumi wa kati jamii ya watanzania kwa kuelewa kuwa  wakiwatendea watanzania ndivyo sivyo adhabu yao itatoka pande mbili kwa Mungu na kwa jamii iliyowachagua.

Ikumbukwe kuwa viongozi wetu waelewe kuwa ni viongozi muhimu sana ambao wataingia katika vitabu vya kumbukumbu ya Taifa hili kuhusu ubora au ubaya kwa Taifa letu.  

swali la kuwauliza Viongozi wetu wa awamu ya tano Je watendaji wake watampa Kaisari yaliyo ya Kaisari  ili kutimiza yale waliokuwa wamehaidi wakati wa kampeni ili kubadilisha maisha ya watanzania?

Je Viongozi wa awamu ya Tano chini ya mwitikio wa Hapa Kazi Tu chini ya DR. Magufuli   wanafahamu ukubwa na umuhimu wa maamuzi yao kwa jamii ya Tanzania?

Je viongozi wetu wa awamu ya tano  wametawaliwa na maadili gani katika utendaji wa kazi yaokuendesha serikali? Ni ukweli usio fichika kuwa ili waweze kufanikiwa katika kutumiza maendeleo ya wananchi
ni lazima wazingatia maadili ya msingi ya kufanikisha  na kusimamia kwa weledi mkubwa falfasa ya Mpe kaizari yaliyo ya kaizari hasa katika kipengele ya ukusanyaji kodi ili kuimalisha mfuko wa serikali kwa maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Rais Dr Magufuli ameonyesha nia dhabiti katika kutekeleza falfasa hii kwa kuanza kutumbua majipu na kupaisha makusanyo ya kodi katika mwezi huu wa December 2015. Kama taifa tunafarijika kuwa timu nzima ya serikali kwa nia nzuri sasa wanawajibika na kuwawajibisha wale wote ambao walikuwa wanakwenda kinyume na falfasa hii ambayo Yesu aliwambia wafarisayo kuhusu dhana ya kutoa kodi.

Tunaendelea kufarijika kila siku njisi watendaji wakuu wa serikali wanavyowajibika sasa na kuruduisha imani kwa Watanzania masikini kuhusu mabadiliko ya maisha yao na jamii nzima. Hivyo ni vyema waendelee kutimiza wajibu badala ya kujali maslahi yao binafsi yatokanayo na itikadi au faida ambayo wanafikiria wao tu watanufaika nayo na sio taifa;

Daima Rais wetu ameendelee kusisitiza kuwa Tanzania niyetu sote na rasilimali ambazo tumejaliwa ni zetu sote na sio mali ya kikundi Fulani tu. Na ameendelea kusisitiza kuwa  anafafahamu wananchi wanatamani nini; wanatamani watoto wao wapate elimu bora ndio maana sasa serikali imerudisha tena elimu bure kwa watoto wetu;

Anajua watanzania wanataka umoja  ndio maana anaendelea kuhubiri na kuwaomba  wananchi kuendelea kudumisha amani iliyopo katika pande zote mbili za jamuhuri ya Muungano;

Hebu tujikumbushe Busara za Baba wetu wa Taifa  Mwalimu Nyerere alipozungumzia dhana ya uongozi, Mwalimu Nyerere alisema, “uongozi ni kuonyesha njia.” Kwa maana hiyo, viongozi shurti wafahamu vyema matokeo ya uongozi wao. Wasome imani za wanaowaongoza na nyakati zilizopo ili kutambua matumaini ya umma kimaisha.

VIONGOZI GANI TUNAWAHITAJI?

Amabao hawawezi jisahau wamepewa dhamana ya  kushika hatamu ya uongozi la msingi hapa ni kuwa kiongozi amabye yuko tayari kuongoza na  na ajuwe anabeba jukumu la kubadilisha hali za watu kuwa nzuri. Atumie stadi za uongozi mwema kuonyesha njia. Mheshimiwa Dr. Magufuli ameweza kulionyesha hili kuwa kiongozi ambaye anajali Taifa na sio kukitumikia kikundi Fulani.

Wanaepuka kutumia stadi za uongozi kusimamia haki za waliowa wafikisha hapo hasa wanyonge. Wajikumbushe kuwa kupewa uongozi ni kuchukua ahadi ya kutenda kwa haki. Ukitaka kulitendea haki jipu lazima ulikamue na ulikamue vizuri na kuhakikisha kuwa kiini kimetoka ili kumpa nafuu mgonjwa. Ugonjwa ambao kama taifa tunao kwa sasa ni uchumi wetu ambao hauendani na maisha ya wananishi wetu. Tunashkukuru majipu haya sasa yanaendelea kutumbuliwa na mgojwa wetu uchumi anaendelea kuimarika.


Mwalimu Nyerere aliandika miongozo mizuri katika Azimio la Arusha miongoni mwao  akisema kwamba ili tuendelee tunahitaji Siasa Safi na Uongozi Bora. Alitambua mchango wa mambo hayo katika maendeleo ya mwanadamu. Kupitia siasa safi kila kitu cha kunufaisha wananchi hupatikana. Bali ni muhimu viongozi wanaotarajiwa kufanikisha ustawi wa wanadamu, wapatikane kwa njia ya haki. Watokane na ridhaa ya watu wenyewe wanaotaka kuongozwa. Na wakisha chaguliwa anatende kazi kwa uadilifu na ustadi mkubwa. Waweze kukusimai uchumi wetu kwa kuhakikisha kuwa yaliyo ya Kaizari anapewa Kaizari kwa faida ya Taifa nzaima.


Watendaji wetu timizeni wajibu wenu ili muweze kumsaidia rais wetu katika kufanikisha adhima ya kulijenga taifa letu kiuchumi kwa faiada ya vizazi vyetu

Mungu ibariki Tanzania

Friday, December 4, 2015

NIMEKUJA KIJIFUNZA KAULI YA WAZIRI MKUU MAJALIWA KASSIM MAJALIWA.



Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa ni waziri mkuu wa awamu ya Tano ambaye anaendana na kasi ya utendaji wa kazi wa Rais wa awamu ya tano Mheshimiwa Dr. Magufuli katika kurudisha uwajibikaji na matumizi mazuri ya fedha za watanzania katika idara za serikali na mashirika ya umma.

Katika hiki kipindi kifupi akiwa kama waziri mkuu ameweza kuonyesha nia dhabiti ya kuwatumikia watanzania wanyonge ambao kwa kipindi kirefu sasa wamekuwa masikini katika taifa lao ambalo lina utajiri mkubwa ambao ulikuwa ukiishia amikanoni mwa wachache.

Ameanza kazi kwa kutembelea au kufanya ziara za ghafla katika idara nyeti za serikali ambazo ni nguvu ya uchumi wa Taifa na daraja pekee katika kuondoa umasikini wa watanzania wanyonge . kauli ya ambayo alitoa hivi karibuni kuwa amekuja tu kujifunza bila kuhitaji maelezo zaidi ilikuwa ni nzito ambayo kwa kweli watendaji wa serikali na idara zake wanatakiwa kuizingatia na kuwa tayari kuwajibika mara moja.

Mheshimiwa Majaliwa ameonyesha ujasiri wake wa kujifunza nini kinaendelea katika utendaji wa watumishi wa serikali na uma na tayari ameanza kuyapa mgongo mazoea ya kale.  Kwa mhesjimiwa majaliwa ambaye hakuwa maarufu sana katika siasa za Tanzania sasa kwa kushirikiana na mhemishimiwa Rais Magufuli kwa pamoja wameamua kuhakikisha wanabadilisha mifumo ambayo ilikuwa inawanyima watanzania kaktika kuyafikia maendeleo kammili, Lengo kubwa la serikali ya tano chini ya Rais, Magufui, Makamu wa rais Samia Suluhu Hassan na Waziri mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa ni kuona kuwa wanabadilisha mifumo yote mibovu  ili kuifanya Tanzmi kuifanya inakuwa bora zaidi kwenye masuala ya uchumi, utawala na maisha ya watanzania masikini.
Waziri Mkuu kwa kushirikia na Uongozi wa awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli wana kila nafasi sasa ya kuandika historia kwa kutumia kauli mbio ya hapa kazi tu na kuhakikisha wanabadilisha mifumo yote mibovu ya kuendesha nchi kwa fiada ya watanzania  
Tukubali kuwa Tanzania ya leo inaweza kuwa tofauti sana na ya jana, na ya kesho ikawashangaza hata watu wa dunia.  Kama Mheshimiwa Majaliwa katika nafasi yake ataweza kuhakikisha kuwa anajenga mfumo ambao, hata kama yeye hatakuwepo madarakani, bado Tanzania na Watanzania watafuata na kuheshimu mifumo mipya itakayowekwa. Ndio maana kauli yake “ nimekuja kujifunza tu ni muhimu sana kwa taifa hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko. Kwa nchi kama ya kwetu, lililo muhimu kwenye mifumo ni kwa wenye kukiuka sheria, kanuni na taratibu zitakazowekwa kuadhibiwa, punde tu wanapokosea.

Je Mheshimiwa Majaliwa amejifunza nini? Na atakuja na somo gani au fundisho gani kwa hao aliowatembelea? Je ataweka mifumo mipya, yenye kutanguliza maslahi ya nchi na si ya watendaji binafsi ambao wameamua kutumia pesa katika kujilipa wao wenyewe? Je hili litakuwa anguko jingine kwa watendaji wabovu ambao wanajali sana masilahi yao na sio ya taifa?,

Kama wengi ambavyo wameseama kuwa kitendo chochote cha kupunguza matumizi yasiyo na lazima, na kutumia fedha kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania lazima kiungwe mkono kwa hali na mali.  Waziri Mkuu Majaliwa anastahili sifa kwa hilo na tumwombee Mungu amlinde ampe nguvu na aweze kutuletea mabadiliko ya kweli. 

Kwangu mimi leo kauli ya “nimekuja kujifunza” ina maana kubwa sana sisi kama taifa tunao wajibu wa kujikomboa kimawazo ili tuweze kufikiri sisi wenyewe, katika kuyapa thamani maamuzi yetu ya utendaji badala ya kusubiri ziara za ghafla za viongozi wetu ili watufundishe jinsi ya kutumia nyazifa zetu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa. Haiingia akili kwa watendaji wa mashirika ya umma pamoja na bozi zake kutumia pesa nyingi ili walipane mishahara na malupulupu binafsi na kuliona shirika linaendelea kudidimia na wafanyakaza na likishindwa kujiendesha. Tuwe na vichwa timamu vya kutuwezesha kuyatafakari masuala sisi wenyewe. Tunapaswa tujijengee huu msingi ili tuweze kuitathmini dhana ya maendeleo, tuweze kujiuliza maendeleo ni nini?

Katika kufanya hivyo, tunapaswa kuchukua jukumu na wajibu wa kujitungia vigezo vyetu na kuvitumia. Lazima tujenge utashi wa kujiamini na kujiamulia mambo yetu wenyewe kwa manufaa  ya taifa letu.  Ni uongo kudhani kuwa hakuna nchi ambayo imesimama tu na haibadiliki. Kosa tunalofanya ni kutozingtia ukweli huo na badala yake kuziona nchi za Ulaya na Marekani kama nchi zilizoendelea na sisi kutumia rasilimali zetu vibaya tukiendelea kusaidiwa na nchi hizo kama sisi ni mataira wa kufikira na hatujui kutenda kazi ipasavyo isipookuwa ni kufikira kuiba tu . Kwa mtindo tulio nao sasa tutabaki na hii dhana ya kujidunisha, na watu wetu kuendelea kuwa masikini miaka yote. Kwa kweli tunatakiwa Kujifunza ili tuweze badilisha huu msimamo tegemezi.

Mheshimiwa Majaliwa anatuonyesha kuwa tuna takiwakuwajibika kujikomboa kifikra, tuweze kujiwekea vigezo vyetu wenyewe. Pasipo kuwa na vigezo vinavyozingatia haki ya  uwajibikaji. Uadilifu na kumwogopa Mungu dhana ya mabadiliko na maendeleo itaendelea kuwa ndoto. Asante awamu ya Tano sasa mmeanza  

kutoondolea dhana hii. Inatubidi tubadili fikra; tukatae huu mkondo uliopo sasa wa kuitwa au kujiita sisi ni masikini wakati watu wachache ambao wamepata nafasi serikalini katika mashirika ya umma kwa sababu zao binafsi wanarudisha maendeleo yetu nyuma.

Dhana ya Maendeleo ni mabadiliko katika kitu au hali yoyote, katika nyanja mbali mbali za maisha, mabadiliko ya manufaa kwa mujibu wa mazingira husika. Katika jamii au nchi, maendeleo yanaboresha maisha ya binadamu, yanahifadhi au kuboresha mazingira, na yanaendana na heshima, utu, na haki. Maendeleo yanatokana na msukumo wa jamii au nchi husika, kwa mujibu wa mahitaji yake halisi, na kwa mujibu wa maamuzi na matakwa ya jamii hiyo, maamuzi yatokanayo na fikra huru na tambuzi, zenye mwelekeo wauwajibikaji na uadilifu. Maendeleo hayatakiwi yalete matabaka miongoni watanzania.

KWA KWELI NIMEKUJA KUJIFUNZA mimi imenifundisha kuwa tukitaka kufanikiwa katika hii safari ya kuondoa umasikini wa Taifa letu tunatakiwa kuendelea kuitekeleza kauli mbiu ya Ya Hapa Kazi Tu kwa vitendo katiaka kujiletea  maendeleo yetu na sisi kama wazalendo wa taifa hili lazima kwa umoja wetu tusiwaonee haya mafisadi, wla rushwa wazembe katika kusukuma gurudumu la nchi yetu mbele , na tuondoe dhana ya kungojea misaada kutoka nchi za nje hii haiwezi kusaidia maendeleo bali inatufanya tuendelee kuwa tegemezi zaidi .

Tunaona mfano wa nchi kama CUBA ile haifuati njia za uchumi kama nchi nyingi duniani ina uchumi wake unaokuwa kila siku , angalia uchina na mipango yao na mao ni serikali ya kikomunisti ndio lakini walikuwa na malengo ikazaa mikakati hii tunayoiona sasa hivi ni dira ya china na kufikia mwaka 2030 iwe super power; au tuangalie nini walifanya south Korea  iaka ile ya 1960s.  
Kwahiyo tuwekeze katika rasilimali ambayo tunajua inaweza kututoa hapa tulipo kwenda hatua mbili au 3 zaidi mbele bila kutegemea msaada kutoka nje. ,

Tunaweza kuendeleza mawazo ma-pya, na kuyakusanya, kuyachuja, kuyaangalia na kuyaunganisha. Hivyo, maendeleo ni hatua ambayo husonga mbele na yenye mabadiliko. Maendeleo yanajumu-isha utendaji ufuatao malengo.  Viongozi wetu wengi wanajiona wao pekee ndio wenye wajibu wa kufaidi utajiri wa nchiyetu, kupitia hulka zao za RUSHWA NA UFISADI.

Sisi kama wananchi wazalendo wa taifa letu tuko tayari kushirikiana na viongozi wa awamu ya tano katika kuyachoma magugu ambayo mengine yalikuwa yameota sugu na kuwa msitu mkubwa ambao umekuwa tishio kwa wachomaji na walulima ambao wako tayari kulisafisha pori hili. Tumeamua kuwaunga Mkono Mheshimiwa Dr. Magufuli Rais wetu na Mama Samia Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Majaliwa msitoke jasho peke yenu katika kufyeka msitu huu. Nasi tjuko tayari kutoa ili shamba letu liweze kutoa mazao bora na sio tene kuitwa shamb la BiBi. Tunafahamu kuwa Shamba la Bibi ni letu sote kila mtu anamchango wa kulifanya listawi na kutoa mazao bora kwa faida ya wajukuu na watoto wote wa Bibi.

 
Kwa kweli nimekuja kujifunza na kugundua kuwa UFISADI NA RUSHWA unatengeneza kikundi cha watu...wenye kusimamia maslahi yao kwa faida yao UFISADI NA RUSHWA Inaunda uwepo wa vikundi visivyo rasimi kisheria kwa ajili ya kupinga/kuzuia/kufanya lobbing na kufanikisha mambo ambayo wao walio kwenye kundi husika Watafaidika nayo;

UFISADI NA RUSHWA Inapanua wigo wa Rushwa kwenye jamii na kufanya baadhi ya watu kwenye jami wasiweze kuguswa na sheria kwa sababu ya uwezo wao kwenye fedha. UFISADI NA RUSHWA Inaleta usumbufu kwenye utendaji wa Serikali kwa kuwa baadhi ya raia wanakuwa na nguvu ya fedha hivyo umma wa raia wa kawaida unatengeneza hofu ya kuogopa watu wao wenye ukwasi.

UFISADI NA RUSHWA Inavunja na kuharibu mfumo wa HAKI kwa kuwa wenye UKWASI huo wa kifisadi wanatumia ukwasi huo kuvulugu HAKI inapotafutwa. UFISADI NA RUSHWA Uzalisha kiburi/Jeuri za watu wenye ukwasi dhidi ya Watumishi wa Umma na kuwafanya waonekane si kitu mbele ya sura za jamii UFISADI NA RUSHWA Uchochea kwa kasi kubwa ongezeko la kukosekana kwa maadili ya umma na maadili ya Viongozi wa umma.Hivyo kuongeza mpasuko wa kuwa Taifa lina mmomonyoko wa maadili.

UFISADI NA RUSHWA Usababisha woga wa kitaifa hata uwezo wa kitaifa kukemea mambo yasiyostahiki utegemea ujasili wa mkemeaji. UFISADI NA RUSHWA Pia utengeneza ushawishi wa wageni kuona sehemu za kupenyeza mambo yao kwa kuwa utafuta milango ya kuingia kwa namna ambayo wao wanaona kuna njia ama upenyo. UFISADI NA RUSHWA Uchafua pia mfumo wa uendeshaji wa siasa na Serikali kwa kujalibu kuweka mapandikizi yake. 

MUNGU IBARIKI TANZANIA KATIKA AWAMU HII YA TANO HAPA KAZI TU 



Wednesday, December 2, 2015

UTHUBUTU WA RAISI MAGUFULI NA UTUMBUAJI MAJIPU



Katika kipindi chote cha Kampeni Mheshimiwa Dr. Magufuli daima alionyesha upendo, maumivu  na haja ya kuibadilisha Tanzania kuwa kweli ya watanznaia na sio Tanzania ya wachache katika kufurahia matunda yatokanayo na rasilimali la taifa letu. Mfuatiliaji mzuri aliweza kugundua kuwa Magufuli aliamua kwa hiari yake kuwatumikia watanzania kuwa kiongozi mzuri kufuatia kwa ajili ya watanzania wote bila ubaguzi wowote.

Rekodi zake za utendaji kwa falfasa ya kuwa atakuwa kiongozi ambaye  hataficha chochote kwa wananchi; hatasema uongo,  na atafichua uongo kila unapoibuka. hatakuwa mtu wa kuficha matatizo, makosa, mapungufu na kushindwa kuyatafutia suluhu na kamwe sio mtu wa makundi au wa kujijengea sifa nyepesi nyepes binafsi.

Mchakamchaka ambao anaendlea kuufanya Magufuli sasa ndicho haswa kinachotakiwa kufanyika katika kipindi kirefu nyuma. Kwa kufanya hivyo, Magufuli anaonyesha wazi kuwa anajua matatizo na mapungufu yaliyopo na badala ya kuyafunika na kuyapaka rangi anayaweka wazi kwa maendeleo ya watanzania wote. Bahati nzuri Magufuli amekuwa akielezea namna atakavyoshughulikia hayo matatizo na mapungufu. Bahati nzuri tabia hii ya Magufuli siyo mpya. Watanzania watakumbuka kuwa hulka hii ya Magufuli ilijionyesha wakati hata alipokuwa waziri chini ya Rais Benjamin Mkapa alipoikosoa Ofisi yake hadharani kwa baadhi ya watumishi wa ofisi hiyo kujimilikishia magari ya umma isivyo halali. Tukumbuke hata Katika kipindi cha kampeni, Magufuli amekuwa akitoa mapungufu ya serikali hata pale ambapo Rais Kikwete yupo.
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuandika kitabu mwaka 1962 kiitwacho "Tujisahihishe" akitaka Watanzania na hasa viongozi wawe tayari muda wote kujisahihisha. Katika kitabu hicho Baba wa Taifa, alisema kuwa “makosa ni makosa bila kujali ni nani ameyafanya. Muhimu ni kuyajua makosa hayo na kujisahihisha.” Katika kitabu hicho, Mwalimu Nyerere aliendelea kusema;

“Kujielimisha ni kujua ukweli wa mambo na kuwa na ujuzi wa sababu mbalimbali za mambo; na kama mambo hayo ni mabaya ni kujua jinsi ya kuyaondoa; na kama ni mema, jinsi ya kuyadumisha. Mpumbavu ni yule anayeyapa mambo sababu zisizo za kweli na kushauri dawa isiyo ya kweli katika kutafuta sababu za matatizo na jinsi ya kuyaondoa(Nyerere, 1962, 5).”

Kwa maelezo hayo ya Baba wa Taifa, ni wazi kuwa Magufuli ameamua kuwa mkweli katika utendaji wake kama Rais wa wamu ya tano na ameepuka kuwa mpumbavu kama alivyobainisha Baba wa Taifa. Magufuli anaamini dhana hii kiongozi mkweli na aliye na uthubutu wa kujikosoa anaonyesha kuwa ana uwezo wa kutafuta suluhisho la kweli la matatizo yaliyopo, na tumejionea katika kipindi kifupi sana akiwa ameanza kutumbua majipu kama alivyohaidi.



kama mwandishi Maggid alivyowahi andika kuwa Sehemu kubwa ya matatizo ya nchi zetu hizi yanatokana na ubinafsi huo. Na bahati mbaya kabisa, baadhi ya viongozi tuliowapa dhamana za uongozi ndio wenye kuongoza kwa matendo yenye kutanguliza maslahi yao binafsi. Kwetu sisi Watanzania hali yetu ya kiuchumi bado duni mno. Ufisadi unalitafuna taifa letu. Tuna lazima ya kukumbushana ukweli huu, maana, tukifanya masihara taifa letu liko katika hatari ya kuingia katika hali ya machafuko makubwa. Ili kuunusuru uchumi wetu usiyumbe zaidi tuna lazima ya kutumia fedha na rasilimali zetu kwa busara kubwa. Kuna busara ya kutomuiga tembo kwa lolote lile

Sokoine alionyesha moyo wa kujitoa kuwatumikia wananchi mara tu baada ya kuteuliwa katika wadhifa wa waziri mkuu wakati huo akiwa mbunge wa Monduli mkoani Arusha. Katika utawala wake, kama waziri mkuu, aliendesha na kusimamia mwenyewe vita dhidi ya dhuluma iliyokuwa inaendeshwa na wachache wenye nacho dhidi ya wengi wasionacho. Vita dhidi ya walanguzi na wahujumu uchumi ni miongoni mwa mambo ambayo yaliinua jina la Sokoine kila pembe ya nchi hii na katika medani za kisiasa.


Sokoine alipenda haki, aliona ni kitu cha kushangaza kwamba wananchi walio wengi walikuwa wanaishi maisha ya dhiki, hawakusikilizwa na watendaji. Alishangaa kuona kwamba urasimu umezama kwenye rushwa za nipe-nikupe na kuporomoka kwa maadili hasa upungufu mkubwa katika kutoa huduma na haki. Sokoine alitumia uwezo kama waziri mkuu kujaribu kurejesha nidhamu katika sekta ya utawala kwa kuwajibisha viongozi na watendaji wabovu. Kwa upande mwingine, alijitahidi kuvunja ushirikiano kati ya viongozi warasimu na wafanyabiashara ambao kwa pamoja waligeuza sekta ya umma kama shamba la bibi. Hili ndilo analolifanya Magufuli na watendaji wake katika mwezi huu wa kwanza wa awamu yake ya Tano ya kuliongoza Taifa hili.

Dr. Magufuli tuko alipopendekezwa na chama chake cha mapinduzi kupeperusha bendera ya kuwania urais wa awamu ya tano alisema wazi kabisa kuwa wananchi wategemee  utumishi uliotukuka toka kwake, watarajie uadilifu wa khali ya juu,watarajie uchapakazi, watarajie serikali itakayo kuwa imara: itakayo simamia maslahi ya uma; na wategemee nidhamu sio tu kwa watumishi wa serikali bali kwa watanzania wote; wasitegemee propaganda za ujanja ujanja; balo ukweli wakati wote; na alihaidi kufuatilia mambo mengi kwa kina mimi  mwenyewe; wasitarajie sherehe na hafla nyingi toka kwangu. Na watarajie kuwa nitalinda umoja amani na usalama wan chi yetu kwa nguvu yetu zote. Nitakuwa kiongozi wa wote bila kubagua mkoa kanda dini kabila wala vyama.

Kama mwandishi Mmoja alivyowahi andika “Dr John Pombe Magufuli raisi wa awamu ya tano anataka kuwaonyesha watanzania kwa ujumla wake kuwa atakaye aliyethubutu kuchezea shilingi ya Serikali atajitutia yeye mwenyewe; ni kweli ilikuwa inasikitisha kila siku kusoma magazeti yenye vichwa vya habari, Mamilioni yametafunwa yayeyuka na kuunda kamati ambazo zilikuwa vile vile zikitumia pesa katika kutafuta suluhu na suluhu haipatikani. Kama mwandishi Maggid alivyowahi andika  Maana, kuna walioishi wakiamini, kuwa ng'ombe wa Serikali huzikwa na ngozi yake. Ni nani anayejali? Maana, kama ng'ombe ni wa mtu binafsi, basi, akifa, atahakikisha walau anachuna ngozi yake, ili walau aambulie senti kidogo! Utamaduni huu wa kudhibiti mapato ya hazina ni utamaduni mwema utakaomsaidia mwananchi wa kawaida”.


Hatua ambazo ampaka sasa rais Dr Magufuli, ameshchukua ni funzo tosha kwa watu wengine; tunafahamu kuwa kuteuliwa na hatimaye kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa awamu ya tono kulitokana sana na record yake ya uchapakazi, uadilifu, kutoyumbishwa hovyo hovyo kwa sababu ya kusimamia kile anachokiamini kwa manufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla, Hiyo imejidhihirisha zaidi katika wizara zote alizowahi kuziongoza mfano Ujenzi na Miundombinu pamoja na Kilimo na ufugaji. Ni kweli kuwa fundisho tunalopata hapa ni kwamba usingoje mpaka upewe nafasi kubwa ya utumishi ndio uanze kuonyesha namna ya kuwatumikia wananchi.


Dr Magufuli ni visionary leader ambaye anaamini katika jambo moja kuwa mabadiliko ya maisha bora yanawezekana  katika Tanzania yetu. Tatizo ambalo analijua linalokwamisha maisha bora kwa watanzania ni Usimamizi mbovu sekta zote kutokana na ubinafsi, udugu, rushwa. Katika kampeni yake alipotembelea kaburi la hayati sokoine alisifu weledi wa hayati sokoine ambaye alikuwa mkweli, mchukia rushwa, na alikuwa na uthubutu bila kumwogopa kiongozi yeyote Edward Moringe Sokoine alikuwa kiongozi mwenye uthubutu wa dhahiri katika kupigania na hata kufia maslahi ya raia, hasa maskini. Tunamkumbuka Moringe alivyowasha moto  bungeni kabla ya kuondoka, hasa alipozungumza kuhusu kubana matumizi ya serikali, ambako kuliambatana na hoja juu ya ukubwa wa serikali na hasa mantiki ya kuwa na mawaziri wasiokuwa na wizara maalum, lakini wakipatiwa haki zote sawa na mawaziri wenye wizara. Nyota yake ilizidi kung'ara na kuwa chachu ya kupendwa miongoni mwa walio wengi; akaonekana mwiba kwa walafi na wadokozi wa keki ya taifa.  

Ingawa kwa upande mmoja Sokoine alionyesha kupata mafanikio kwa kuungwa mkono na wananchi, kwa upande mwingine alijikuta akipoteza marafiki na kujijengea maadui lukuki kutokana na mfumo wa utendaji uliokuwepo kabla yake. Katika utendaji wake mara zote, Sokoine aliamini katika siasa za uwazi. Alizungumza kile alichoamini ndicho na alisimamia na alionyesha mfano katika utekelezaji wa kila jambo alilotaka lifanyike. Mambo mengi aliyojaribu kufanya Sokoine yalitokana na uthubutu wake binafsi. Alitumia mfano wake kama kiongozi ambaye alikuwa na uadilifu mkubwa na hakuwa na ubinafsi.

Rekodi ya utendaji kazi wa kiongozi huyu ambaye alibahatika kushika wadhifa wa waziri mkuu katika vipindi viwili tofauti, haijafikiwa na kiongozi yeyote katika ngazi hiyo, miongo mitatu tangu kifo chake. Inasemekana ni katika kipindi chake cha uongozi, Mwalimu Nyerere alipata ahueni, alinenepa. 



Na katika awamu hii ya Magufuli watanzania wanyonge ni zamu yao kunenepa; na kuanza kufurahia matunda ya nchi yao tumejionea wenyewe muhimbili wagonjwa wakiwa wamelala katika vitanda na sio katika sakafu.



Kama ilivyokuwa kwa marehemu  Sokoine Mheshimiwa Dr. Magufuli ameanza kuonyesha kuwa atakuwa kiongozi mkuu ambaye ataweza kuisimamia kusimamia serikali kwani ameonyesha kwa moyo mkunjufu kuwa anamainisha kila ambacho anakiongelea na kukiishi. Tunafahamu kuwa viongozi wa aina ya Mwalimu Nyerere na Sokoine hawazaliwi kila mara. Kama taifa tumepata bahati ya ajabu kwani sasa tumempata kiongozi wa aina hii ndio mheshimiwa Dr.John Pombe Joseph Magufuli. Amekuwa kiongozi mwenye ujasiri wa kuchukua maamuzi katika mazingira magumu ambayo yanawagusa hata vigogo wa serikali ili nguvu kubwa zielekezwe kuwasaidia maskini,.


Dr. Magufuri ameonyesha awajibike wa ukweli, kuwa muwazi katika utendaji wake kubana matumizia ya serikali.

Maswali ambayo najiuliza leo

  • Uwajibikaji ulipotelea wapi kwa viongozi wetu?


  • Nini maana ya kuwa kiongozi wa umma?


  •  Je wengi wa viongozi wetu wanaelewa dhana hii nzima ya kuutumikia umma au jamii?


  • Je walioko madarakani na wanaoongozwa wanaonyesha na kufahamu wajibu wao kwa jamii na kuwa viongozi bora wa kuigwa na kizazi chetu cha baadae?


Ninachofurahia mimi katika awamu hii ya tano, misamiati kama kula nchi kwa watendaji wa serikali na mashirika ya umma; dhana ya umungu mtu kwa watendaji wengi sasa inapotea katika kamusi ya utumishi wa umma.


Ni wakati umefika sasa kwa watendaji wetu kujua nini maana ya uongozi; na wakumbuke kuwa uongozi sio maana yake kulindana katika utendaji wa maovu. Imefika wakati wa kuwaambia viongozi wote wabovu umekosea ondoka:  Mheshimiwa Magufuli ameweza kuonyesha hili katika kipindi kifupi sasa cha uongozi wake kama Rais Magufuli ameonyesha kwa dhati Moyo wa kuwatumikia hao waliomchagua na sio kujali maisha yake na familia yake tu kama ambavyo hali ilivyo sasa. Hivi sasa Dr. Magufuli anaifufua dhana yaw a kuwatumikia wanachi ambayo ilikuwa imeshakufa na kupitwa na wakati. Hapa nchini kwetu kila aingiaye madarakani anafikiria kujinufaisha binafsi na waliomzunguka.

Uongozi na kuwa kiongozi Tanzania ilikuwa ni mradi wa kutajirika na wala hakuna anaeuliza mara baada ya kiongozi kuwa madarakani maisha yake kwa ujumla yanabadilika na kuwa ni mtu wa juu kupita wote ndani ya jamii husika. Inashangaza lakini hii ndio hali halisi kwa Tanzania yetu.  Hatukatai mabadiliko lakini hali iliyoko sasa inakatisha tamaa kwa wanaojua maana ya kuwa kiongozi wa umma.

Nimefurahi kwa ujasili wa Dr. Magufuli wa kuondoa  utamaduni uliojengeka wa kusifia makosa na pale mmoja miongoni mwetu anapotaka kusema ukweli huambiwa ni msaliti wakati anachotaka kukisema au alichosema ni cha haki na ukweli kabisa. Asante Mheshimiwa Magufuli kwa kuanza kuibadili dhana hii na kuwabadili na wananchi kwa ujumla huu sio wakati tena wa kuwaachia watu wachache wakitupeleka peleka katika lindi la umasikini na matatizo kutokana na ubinafsi na ulafi wao tu.

Mheshimiwa Magufuli amesema kuwa kazi  iliyo mbele yake ni kubwa na ngumu lakini amekubali kuwa yeye ndiye atakuwa anatumbua haya majipu; hivyo Kama Mwandishi mmoja aliandika kuwa “ Uzalendo wetu kama Watanzania tunaoipenda nchi hii ni kubainisha yale machafu ya viongozi na sio kuwa wanafiki. Ilishasemwa zamani kuwa Ukweli ni mchungu, hatuna budi kuusema japo unauma tuseme ukweli bila ya hivyo matatizo yetu hayawezi kwisha kwa kutegemea wanafiki na walioingia madarakani kwa maslahi binafsi”

Maendeleo ya kweli ya watanzania yatatoka na watanzania wenyewe; Hata siku moja hatotokea mtu toka nje ya nchii hii kuja kutuletea maendeleo ila ni sisi wenyewe tunapaswa kujiletea hayo maendeleo, nayo ni kuwajibika kutokana na dhamana tulizopewa na sio kuipelekea kuzimu nchi yetu kama hali ilivyo sasa. Mfano mdogo tu hebu angalia uozo wa Bandari na TRA na hasara ambayo Taifa limepata.


Mheshimiwa Rais Magufuli ameliona wazi kuwa Kiongozi wa umma anawajibika kwa umma uliomuweka madarakani na sio kufanya safari nyingi za nje na kusema kuwa hana nafasi  na kwenda vivijini kuona shida za watanzania Hongera Dr. Magufuli kwa kuliona hilo. Uamuzi wa hivi karibuni wa  kufuta safari za nje ni wa kishujaa na utapunguza matumizi makubwa ya pesa za wananchi.  Hii inaonyesha jinsi ya ukubwa wa tatizo la viongozi kutowajibika kutokana na nafasi zao ndani ya nchi hii lilivyo.

Ni wakati umefika sasa wa kuanza upya kuanza kujitawala tukaanza kujenga Taifa la viongozi na wananchi wanaowajibika kutokana na nafasi zao kwa maendeleo ya Taifa hili kama ilivyokuwa kwa viongozi waadilifu kama Mwalimu Nyerere na Edward Moringe Sokoine; Unapowajibika kutokana na nafasi ya uongozi inaonesha ni jinsi gani ulivyokuwa kimaadili na kuwa tayari kulitumikia Taifa la wanyonge.




Tukumbuke kuwa zao la viongozi wabovu limezalisha taifa la Watanzania walio wengi sasa wamejikita katika mazingira ya udanganyifu, rushwa na uzembe.  Tukumbuke kuwa Watumishi wa umma wametakiwa kufanya kazi kwa bidii, uwajibikaji, weledi na ushirikiano ili kuuiwezesha Serikali kuwaletea maendeleo wananchi wake na taifa  kwa ujumla. 

MHESHIMIWA RAIS DR. JOHN POMBE MAGUFULI WATANZANIA TUNAKUOMBEA KATIKA SAFARI HII YA UTUMBUAJI MAJIPU KWA AJILI YA MAENDELEO YA WANYONGE: TANZANIA SIO MASIKINI ILA VIONGOZI WACHACHE AMBAO TULIWAKABIDHI NAFASI MBALIMBALI WALIKIUKA MAADILI YA UONGOZI NA KULILETEA TAIFA HASARA KUBWA.

MUNGU IBARIKI TANZANIA MUNGU MBARIKI RAIS WETU MAGUFULI AENDELEE KUWAHUDUMIA WANYONGE NA MASIKINI -TANZANIA